| ← Romans (3/16) → |
| 1. | Basi Myahudi ana ziada gani? Na kutahiriwa kwafaa nini? |
| 2. | Kwafaa sana kwa kila njia. Kwanza kwa kuwa wamekabidhiwa mausia ya Mungu. |
| 3. | Ni nini, basi, ikiwa baadhi yao hawakuamini? Je! Kutokuamini kwao kutaubatili uaminifu wa Mungu? |
| 4. | Hasha! Mungu aonekane kuwa amini na kila mtu mwongo; kama ilivyoandikwa, Ili ujulike kuwa una haki katika maneno yako, Ukashinde uingiapo katika hukumu. |
| 5. | Lakini, ikiwa udhalimu wetu waithibitisha haki ya Mungu, tuseme nini? Je! Mungu ni dhalimu aletaye ghadhabu? (Nasema kwa jinsi ya kibinadamu.) |
| 6. | Hasha! Kwa maana hapo Mungu atawezaje kuuhukumu ulimwengu? |
| 7. | Lakini, ikiwa kweli ya Mungu imezidi kudhihirisha utukufu wake kwa sababu ya uongo wangu, mbona mimi ningali nahukumiwa kuwa ni mwenye dhambi? |
| 8. | Kwa nini tusiseme (kama tulivyosingiziwa, na kama wengine wanavyokaza kusema ya kwamba twasema hivyo), Na tufanye mabaya, ili yaje mema? Ambao kuhukumiwa kwao kuna haki. |
| 9. | Ni nini basi? Tu bora kuliko wengine? La! Hata kidogo. Kwa maana tumekwisha kuwashitaki Wayahudi na Wayunani ya kwamba pia wamekuwa chini ya dhambi; |
| 10. | kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Hakuna mwenye haki hata mmoja. |
| 11. | Hakuna afahamuye; Hakuna amtafutaye Mungu. |
| 12. | Wote wamepotoka, wameoza wote pia; Hakuna mtenda mema, la! Hata mmoja. |
| 13. | Koo lao ni kaburi wazi, Kwa ndimi zao wametumia hila. Sumu ya fira i chini ya midomo yao. |
| 14. | Vinywa vyao vimejaa laana na uchungu. |
| 15. | Miguu yao ina mbio kumwaga damu. |
| 16. | Uharibifu na mashaka yamo njiani mwao. |
| 17. | Wala njia ya amani hawakuijua. |
| 18. | Kumcha Mungu hakupo machoni pao. |
| 19. | Basi twajua ya kuwa mambo yote inenayo torati huyanena kwa hao walio chini ya torati, ili kila kinywa kifumbwe, na ulimwengu wote uwe chini ya hukumu ya Mungu; |
| 20. | kwa sababu hakuna mwenye mwili atakayehesabiwa haki mbele zake kwa matendo ya sheria; kwa maana kutambua dhambi huja kwa njia ya sheria. |
| 21. | Lakini sasa, haki ya Mungu imedhihirika pasipo sheria; inashuhudiwa na torati na manabii; |
| 22. | ni haki ya Mungu iliyo kwa njia ya imani katika Yesu Kristo kwa wote waaminio. Maana hakuna tofauti; |
| 23. | kwa sababu wote wamefanya dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu; |
| 24. | wanahesabiwa haki bure kwa neema yake, kwa njia ya ukombozi ulio katika Kristo Yesu; |
| 25. | ambaye Mungu amekwisha kumweka awe upatanisho |
| 26. | apate kuonyesha haki yake wakati huu, ili awe mwenye haki na mwenye kumhesabu haki yeye amwaminiye Yesu. |
| 27. | Ku wapi, basi, kujisifu? Kumefungiwa nje. Kwa sheria ya namna gani? Kwa sheria ya matendo? La! Bali kwa sheria ya imani. |
| 28. | Basi, twaona ya kuwa mwanadamu huhesabiwa haki kwa imani pasipo matendo ya sheria. |
| 29. | Au je! Mungu ni Mungu wa Wayahudi tu? Siye Mungu wa Mataifa pia? Naam, ni Mungu wa Mataifa pia; |
| 30. | kama kwa kweli Mungu ni mmoja, atakayewahesabia haki wale waliotahiriwa katika imani, nao wale wasiotahiriwa atawahesabia haki kwa njia ya imani iyo hiyo. |
| 31. | Basi, je! Twaibatilisha sheria kwa imani hiyo? Hasha! Kinyume cha hayo twaithibitisha sheria. |
| ← Romans (3/16) → |