← Romans (12/16) → |
1. | Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana. |
2. | Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu. |
3. | Kwa maana kwa neema niliyopewa namwambia kila mtu aliyeko kwenu asinie makuu kupita ilivyompasa kunia; bali awe na nia ya kiasi, kama Mungu alivyomgawia kila mtu kiasi cha imani. |
4. | Kwa kuwa kama vile katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja; |
5. | Vivyo hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake. |
6. | Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema mliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani; |
7. | ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; |
8. | mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia kwa bidii mwenye kurehemu, kwa furaha. |
9. | Pendo na lisiwe na unafiki lichukieni lililo ovu, mkiambatana na lililo jema. |
10. | Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu; |
11. | kwa bidii, si walegevu; mkiwa na juhudi katika roho zenu; mkimtumikia Bwana; |
12. | kwa tumaini, mkifurahi; katika dhiki, mkisubiri; katika kusali, mkidumu; |
13. | kwa mahitaji ya watakatifu, mkifuata ukarimu; katika kukaribisha wageni mkijitahidi. |
14. | Wabarikini wanaowaudhi; barikini, wala msilaani. |
15. | Furahini pamoja nao wafurahio; lieni pamoja nao waliao. |
16. | Mpatane nia zenu ninyi kwa ninyi. Msinie yaliyo makuu, lakini mkubali kushughulishwa na mambo manyonge. Msiwe watu wa kujivunia akili. |
17. | Msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni yaliyo mema machoni pa watu wote. |
18. | Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote. |
19. | Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana. |
20. | Lakini, Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake. |
21. | Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema. |
← Romans (12/16) → |