| ← Psalms (96/150) → |
| 1. | Mwimbieni Bwana wimbo mpya, Mwimbieni Bwana, nchi yote. |
| 2. | Mwimbieni Bwana, libarikini jina lake, Tangazeni wokovu wake siku kwa siku. |
| 3. | Wahubirini mataifa habari za utukufu wake, Na watu wote habari za maajabu yake. |
| 4. | Kwa kuwa Bwana ni mkuu mwenye kusifiwa sana. Na wa kuhofiwa kuliko miungu yote. |
| 5. | Maana miungu yote ya watu si kitu, Lakini Bwana ndiye aliyezifanya mbingu. |
| 6. | Heshima na adhama ziko mbele zake, Nguvu na uzuri zimo katika patakatifu pake. |
| 7. | Mpeni Bwana, enyi jamaa za watu, Mpeni Bwana utukufu na nguvu. |
| 8. | Mpeni Bwana utukufu wa jina lake, Leteni sadaka mkaziingie nyua zake. |
| 9. | Mwabuduni Bwana kwa uzuri wa utakatifu, Tetemekeni mbele zake, nchi yote. |
| 10. | Semeni katika mataifa, Bwana ametamalaki; Naam, ulimwengu umethibitika usitikisike, Atawahukumu watu kwa adili. |
| 11. | Mbingu na zifurahi, nchi na ishangilie, Bahari na ivume na vyote viijazavyo, |
| 12. | Mashamba na yashangilie, na vyote vilivyomo, Ndipo miti yote ya mwituni iimbe kwa furaha; |
| 13. | Mbele za Bwana, kwa maana anakuja, Kwa maana anakuja aihukumu nchi. Atauhukumu ulimwengu kwa haki, Na mataifa kwa uaminifu wake. |
| ← Psalms (96/150) → |