| ← Psalms (88/150) → |
| 1. | Ee Bwana, Mungu wa wokovu wangu Mchana na usiku nimelia mbele zako. |
| 2. | Maombi yangu yafike mbele zako, Uutegee ukelele wangu sikio lako. |
| 3. | Maana nafsi yangu imeshiba taabu, Na uhai wangu umekaribia kuzimu. |
| 4. | Nimehesabiwa pamoja nao washukao shimoni; Nimekuwa kama mtu asiye na msaada. |
| 5. | Miongoni mwao waliokufa nimetupwa, Kama waliouawa walalao makaburini. Hao ambao Wewe huwakumbuki tena, Wametengwa mbali na mkono wako. |
| 6. | Mimi umenilaza katika shimo la chini, Katika mahali penye giza vilindini. |
| 7. | Ghadhabu yako imenilemea, Umenitesa kwa mawimbi yako yote. |
| 8. | Wanijuao umewatenga nami; Umenifanya kuwa chukizo kwao; Nimefungwa wala siwezi kutoka. |
| 9. | Jicho langu limefifia kwa ajili ya mateso Bwana, nimekuita kila siku; Nimekunyoshea Wewe mikono yangu. |
| 10. | Wafu je! Utawafanyia miujiza? Au waliofariki watasimama na kukuhimidi? |
| 11. | Fadhili zako zitasimuliwa kaburini? Au uaminifu wako katika uharibifu? |
| 12. | Miujiza yako itajulikana gizani? Au haki yako katika nchi ya usahaulifu? |
| 13. | Lakini mimi nimekulilia Wewe, Bwana, Na asubuhi maombi yangu yatakuwasilia. |
| 14. | Bwana, kwa nini kuitupa nafsi yangu, Na kunificha uso wako? |
| 15. | Nateswa mimi hali ya kufa tangu ujana, Nimevumilia vitisho vyako na kufadhaika. |
| 16. | Hasira zako kali zimepita juu yangu, Maogofyo yako yameniangamiza. |
| 17. | Yamenizunguka kama maji mchana kutwa, Yamenisonga yote pamoja. |
| 18. | Mpenzi na rafiki umewatenga nami, Nao wanijuao wamo gizani. |
| ← Psalms (88/150) → |