Psalms (85/150)  

1. Bwana, umeiridhia nchi yako, Umewarejeza mateka wa Yakobo.
2. Umeusamehe uovu wa watu wako, Umezisitiri hatia zao zote.
3. Umeiondoa ghadhabu yako yote, Umerudi na kuuacha ukali wa hasira yako.
4. Mungu wa wokovu wetu, uturudishe, Uikomeshe hasira uliyo nayo juu yetu.
5. Je! Utatufanyia hasira hata milele? Utadumisha ghadhabu kizazi hata kizazi?
6. Je! Hutaki kurudi na kutuhuisha, Watu wako wakufurahie?
7. Ee Bwana, utuonyeshe rehema zako, Utupe wokovu wako.
8. Na nisikie atakavyosema Mungu Bwana, Maana atawaambia watu wake amani, Naam, na watauwa wake pia, Bali wasiurudie upumbavu tena.
9. Hakika wokovu wake u karibu na wamchao, Utukufu ukae katika nchi yetu.
10. Fadhili na kweli zimekutana, Haki na amani zimehusiana.
11. Kweli imechipuka katika nchi, Haki imechungulia kutoka mbinguni.
12. Naam, Bwana atatoa kilicho chema, Na nchi yetu itatoa mazao yake.
13. Haki itakwenda mbele zake, Nayo itazifanya hatua zake kuwa njia.

  Psalms (85/150)