Psalms (77/150)  

1. Nimpazie Mungu sauti yangu, Naam, nimpazie Mungu, naye atanisikia.
2. Siku ya taabu yangu nalimtafuta Bwana; Mkono wangu ulinyoshwa usiku, haukulegea; Nafsi yangu ilikataa kufarijika.
3. Nilipotaka kumkumbuka Mungu nalifadhaika; Nilipotaka kutafakari roho yangu ilizimia.
4. Ulizishika kope za macho yangu zisifumbike; Naliona mashaka nisiweze kunena.
5. Nalifikiri habari za siku za kale, Miaka ya zamani zilizopita.
6. Nakumbuka wimbo wangu usiku, Nawaza moyoni mwangu, Roho yangu ikatafuta.
7. Je! Bwana atatupa milele na milele? Hatatenda fadhili tena kabisa?
8. Rehema zake zimekoma hata milele? Ahadi yake imekwisha hata vizazi vyote?
9. Mungu amesahau fadhili zake? Amezuia kwa hasira rehema zake?
10. Nikasema, Ndio udhaifu wangu huo; Lakini nitaikumbuka miaka ya mkono wa kuume wake Aliye juu.
11. Nitayakumbuka matendo ya Bwana; Naam, nitayakumbuka maajabu yako ya kale.
12. Pia nitaitafakari kazi yako yote; Nitaziwaza habari za matendo yako.
13. Ee Mungu, njia yako i katika utakatifu; Ni nani aliye mungu mkuu kama Mungu?
14. Wewe ndiwe Mungu ufanyaye maajabu; Uliudhihirisha uweza wako kati ya mataifa.
15. Kwa mkono wako umewakomboa watu wako, Wana wa Yakobo na Yusufu.
16. Ee Mungu, yale maji yalikuona, Yale maji yalikuona, yakaogopa. Vilindi vya maji navyo vikatetemeka,
17. Mawingu yakamwaga maji. Mbingu nazo zikatoa sauti, Mishale yako nayo ikatapakaa.
18. Sauti ya radi yako ikawa katika kisulisuli; Umeme uliuangaza ulimwengu. Nchi ilitetemeka na kutikisika;
19. Njia yako ilikuwa katika bahari. Na mapito yako yalikuwa katika maji makuu; Hatua zako hazikujulikana.
20. Uliwaongoza watu wako kama kundi, Kwa mkono wa Musa na Haruni.

  Psalms (77/150)