Psalms (68/150)  

1. Mungu huondoka, adui zake wakatawanyika, Nao wamchukiao huukimbia uso wake.
2. Kama moshi upeperushwavyo, Ndivyo uwapeperushavyo wao; Kama nta iyeyukavyo mbele ya moto, Ndivyo waovu wapoteavyo usoni pa Mungu.
3. Bali wenye haki hufurahi, Na kuushangilia uso wa Mungu, Naam, hupiga kelele kwa furaha.
4. Mwimbieni Mungu, lisifuni jina lake, Mtengenezeeni njia ya barabara, Apitaye majangwani kama mpanda farasi; Jina lake ni YAHU; shangilieni mbele zake.
5. Baba wa yatima na mwamuzi wa wajane, Mungu katika kao lake takatifu.
6. Mungu huwakalisha wapweke nyumbani; Huwatoa wafungwa wakae hali ya kufanikiwa; Bali wakaidi hukaa katika nchi kavu.
7. Ee Mungu, ulipotoka mbele ya watu wako, Ulipopita nyikani,
8. Nchi ilitetemeka Naam, mbingu zilidondoka usoni pa Mungu; Hata Sinai usoni pa Mungu; Mungu wa Israeli.
9. Ee Mungu, ulinyesha mvua ya neema; Urithi wako ulipochoka uliutia nguvu.
10. Kabila yako ilifanya kao lake huko; Ee Mungu, kwa wema wako uliwaruzuku walioonewa.
11. Bwana analitoa neno lake; Wanawake watangazao habari ni jeshi kubwa;
12. Wafalme wa majeshi wanakimbia, wanakimbia; Na mwanamke akaaye nyumbani agawa nyara.
13. Kwa nini kulala mazizini arukapo hua, Mbawa zake ziking'aa kama fedha Na manyoya yake kama dhahabu?
14. Mwenyezi Mungu alipotawanya wafalme huko, Kulinyesha theluji katika Salmoni.
15. Ni mlima wa Mungu mlima Bashani, Ni mlima mrefu mlima Bashani.
16. Enyi milima mirefu, kwani kuutazama kwa wivu Mlima alioutamani Mungu akae juu yake? Naam, Bwana atakaa juu yake milele.
17. Magari ya Mungu ni ishirini elfu, maelfu maelfu; Bwana yumo kati yao kama katika Sinai, Katika patakatifu.
18. Wewe umepaa juu, umeteka mateka, Umepewa vipawa katikati ya wanadamu; Naam, hata na wakaidi, Bwana Mungu akae nao.
19. Na ahimidiwe Bwana, Siku kwa siku hutuchukulia mzigo wetu; Mungu ndiye wokovu wetu.
20. Mungu kwetu sisi ni Mungu wa kuokoa; Na njia za kutoka mautini zina YEHOVA Bwana.
21. Naam, Mungu atakipasua kichwa cha adui zake, Utosi wenye nywele wa mtu afulizaye kukosa.
22. Bwana alisema, Kutoka Bashani nitawarudisha, Nitawarudisha kutoka vilindi vya bahari;
23. Uuchovye mguu wako katika damu ya adui zako, Na ulimi wa mbwa zako upate sehemu yake.
24. Ee Mungu, wameiona miendo yako; Miendo ya Mungu wangu, Mfalme wangu, katika patakatifu
25. Waimbaji hutangulia, nyuma yao wapigao vinanda, Kati ya wanawali wapiga matari.
26. Mhimidini Mungu katika mikutano, Bwana katika makusanyiko ya Israeli.
27. Yuko Benyamini mdogo, mtawala wao; Wakuu wa Yuda, kundi lao; Wakuu wa Zabuloni; Wakuu wa Naftali.
28. Ee Mungu, uziamuru nguvu zako; Ee Mungu, uwe hodari uliyetufanyia makuu.
29. Kwa ajili ya hekalu lako Yerusalemu Wafalme watakuletea hedaya.
30. Mkemee mnyama wa manyasini; Kundi la mafahali, na ndama za watu; Hata wanyenyekee na kuleta vipande vya fedha, Uwatawanye watu wapendao vita.
31. Masheki watakuja kutoka Misri, Kushi itamnyoshea Mungu mikono yake mara.
32. Enyi falme za dunia, mwimbieni Mungu, Msifuni Bwana kwa nyimbo.
33. Apandaye mbingu za mbingu za tangu milele; Aitoa sauti yake, sauti ya nguvu.
34. Mhesabieni Mungu nguvu; Enzi yake i juu ya Israeli; Na nguvu zake zi mawinguni.
35. Mungu ni mwenye kutisha Kutoka patakatifu pako. Ndiye Mungu wa Israeli; Yeye huwapa watu wake nguvu na uwezo. Na ahimidiwe Mungu.

  Psalms (68/150)