| ← Psalms (65/150) → |
| 1. | Ee Mungu, sifa zakulaiki katika Sayuni, Na kwako Wewe itaondolewa nadhiri. |
| 2. | Wewe usikiaye kuomba, Wote wenye mwili watakujia. |
| 3. | Ingawa maovu mengi yanamshinda, Wewe utayafunika maasi yetu. |
| 4. | Heri mtu yule umchaguaye, Na kumkaribisha akae nyuani mwako. Na tushibe wema wa nyumba yako, Patakatifu pa hekalu lako. |
| 5. | Kwa mambo ya kutisha utatujibu, Katika haki, Ee Mungu wa wokovu wetu. Wewe uliye tumaini la miisho yote ya dunia, Na la bahari iliyo mbali sana, |
| 6. | Milima waiweka imara kwa nguvu zako, Huku ukijifunga uweza kama mshipi. |
| 7. | Wautuliza uvumi wa bahari, Uvumi wa mawimbi yake, Na ghasia ya mataifa; |
| 8. | Kwa hiyo wakaao mbali kabisa huogopa ishara zako; Milango ya asubuhi na jioni waifurahisha. |
| 9. | Umeijilia nchi na kuisitawisha, Umeitajirisha sana; Mto wa Mungu umejaa maji; Wawaruzuku watu nafaka Maana ndiwe uitengenezaye ardhi. |
| 10. | Matuta yake wayajaza maji; Wapasawazisha palipoinuka, Wailainisha nchi kwa manyunyu; Waibariki mimea yake. |
| 11. | Umeuvika mwaka taji ya wema wako; Mapito yako yadondoza unono. |
| 12. | Huyadondokea malisho ya nyikani, Na vilima vyajifunga furaha. |
| 13. | Na malisho yamevikwa kondoo, Na mabonde yamepambwa nafaka, Yanashangilia, naam, yanaimba. |
| ← Psalms (65/150) → |