Psalms (64/150)  

1. Mungu, uisikie sauti yangu katika malalamiko yangu; Unilinde uhai wangu na hofu ya adui.
2. Utanificha mbali na shauri la siri la watenda mabaya, Mbali na ghasia ya watu wafanyao maovu;
3. Waliounoa ulimi wao kama upanga, Wameielekeza mishale yao, maneno ya uchungu,
4. Wapate kumpiga mkamilifu faraghani, Kwa ghafula humpiga wala hawaogopi.
5. Walijifanya hodari katika jambo baya; Hushauriana juu ya kutega mitego; Husema, Ni nani atakayeiona?
6. Hutunga maovu; husema, Tumefanya shauri kamili; Na mawazo ya ndani ya kila mmoja wao, Na moyo wake, huwa siri kabisa.
7. Kwa hiyo Mungu atawapiga shabaha, Kwa mshale mara watapigwa.
8. Ndivyo watakavyokwazwa, Ulimi wao wenyewe ukishindana nao. Wote wawaonao watatikisa kichwa.
9. Na watu wote wataogopa, Wataitangaza kazi ya Mungu, Na kuyafahamu matendo yake.
10. Mwenye haki atamfurahia Bwana na kumkimbilia, Na wote wenye moyo wa adili watajisifu.

  Psalms (64/150)