| ← Psalms (63/150) → |
| 1. | Ee MUNGU, Mungu wangu, nitakutafuta mapema, Nafsi yangu inakuonea kiu, Mwili wangu wakuonea shauku, Katika nchi kame na uchovu, isiyo na maji. |
| 2. | Ndivyo nilivyokutazama katika patakatifu, Nizione nguvu zako na utukufu wako. |
| 3. | Maana fadhili zako ni njema kuliko uhai; Midomo yangu itakusifu. |
| 4. | Ndivyo nitakavyokubariki maadamu ni hai; Kwa jina lako nitaiinua mikono yangu. |
| 5. | Nafsi yangu itakinai kama kushiba mafuta na vinono; Kinywa changu kitakusifu kwa midomo ya furaha. |
| 6. | Ninapokukumbuka kitandani mwangu, Nakutafakari Wewe makesha yote ya usiku. |
| 7. | Maana Wewe umekuwa msaada wangu, Na uvulini mwa mbawa zako nitashangilia. |
| 8. | Nafsi yangu inakuandama sana; Mkono wako wa kuume unanitegemeza. |
| 9. | Bali waitafutao nafsi yangu, ili kuiharibu, Wataingia pande za nchi zilizo chini. |
| 10. | Watatolewa wafe kwa nguvu za upanga, Watakuwa riziki za mbwa-mwitu. |
| 11. | Bali mfalme atamfurahia Mungu, Kila aapaye kwa Yeye atashangilia, Kwa maana vinywa vya waongo vitafumbwa. |
| ← Psalms (63/150) → |