Psalms (62/150)  

1. Nafsi yangu yamngoja Mungu peke yake kwa kimya, Wokovu wangu hutoka kwake.
2. Yeye tu ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana.
3. Hata lini mtamshambulia mtu, Mpate kumwua ninyi nyote pamoja? Kama ukuta unaoinama, Kama kitalu kilicho tayari kuanguka,
4. Hufanya shauri kumwangusha tu katika cheo chake; Huufurahia uongo. Kwa kinywa chao hubariki; Kwa moyo wao hulaani.
5. Nafsi yangu, umngoje Mungu peke yake kwa kimya. Tumaini langu hutoka kwake.
6. Yeye tu ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana.
7. Kwa Mungu wokovu wangu, Na utukufu wangu; Mwamba wa nguvu zangu, Na kimbilio langu ni kwa Mungu.
8. Enyi watu, mtumainini sikuzote, Ifunueni mioyo yenu mbele zake; Mungu ndiye kimbilio letu.
9. Hakika binadamu ni ubatili, Na wenye cheo ni uongo, Katika mizani huinuka; Wote pamoja ni hafifu kuliko ubatili.
10. Msiitumainie dhuluma, Wala msijivune kwa unyang'anyi; Mali izidipo msiiangalie sana moyoni.
11. Mara moja amenena Mungu; Mara mbili nimeyasikia haya, Ya kuwa nguvu zina Mungu,
12. Na fadhili ziko kwako, Ee Bwana; Maana ndiwe umlipaye kila mtu Sawasawa na haki yake.

  Psalms (62/150)