| ← Psalms (55/150) → |
| 1. | Ee Mungu, uisikilize sala yangu, Wala usijifiche nikuombapo rehema. |
| 2. | Unisikilize na kunijibu, Nimetanga-tanga nikilalama na kuugua. |
| 3. | Kwa sababu ya sauti ya adui, Kwa sababu ya dhuluma yake yule mwovu. Kwa maana wananitupia uovu, Na kwa ghadhabu wananiudhi. |
| 4. | Moyo wangu unaumia ndani yangu, Na hofu za mauti zimeniangukia. |
| 5. | Hofu na tetemeko limenijia, Na hofu kubwa imenifunikiza. |
| 6. | Nikasema, Ningekuwa na mbawa kama njiwa, Ningerukia mbali na kustarehe. |
| 7. | Ningekwenda zangu mbali, Ningetua jangwani. |
| 8. | Ningefanya haraka kuzikimbia Dhoruba na tufani. |
| 9. | Ee Bwana, uwaangamize, uzichafue ndimi zao, Maana nimeona dhuluma na fitina katika mji. |
| 10. | Mchana na usiku huzunguka kutani mwake; Uovu na taabu zimo ndani yake; |
| 11. | Tamaa mbaya zimo ndani yake; Dhuluma na hila haziondoki mitaani mwake. |
| 12. | Kwa maana aliyetukana si adui; Kama ndivyo, ningevumilia. Aliyejitukuza juu yangu siye anichukiaye; Kama ndivyo, ningejificha asinione. |
| 13. | Bali ni wewe, mtu mwenzangu, Rafiki yangu, niliyejuana nawe sana. |
| 14. | Tulipeana shauri tamu; na kutembea Nyumbani mwa Mungu pamoja na mkutano. |
| 15. | Mauti na iwapate kwa ghafula, Na washuke kuzimu wangali hai, Maana uovu u makaoni mwao na katikati yao. |
| 16. | Nami nitamwita Mungu, Na Bwana ataniokoa; |
| 17. | Jioni, asubuhi, na adhuhuri nitalalama na kuugua, Naye ataisikia sauti yangu. |
| 18. | Ameiokoa nafsi yangu iwe salama, asinikaribie mtu, Maana walioshindana nami walikuwa wengi. |
| 19. | Mungu atasikia na kuwajibu; Ndiye Yeye akaaye tangu milele. Mageuzi ya mambo hayawapati hao, Kwa hiyo hawamchi Mungu. |
| 20. | Amenyosha mkono awadhuru waliopatana naye, Amelihalifu agano lake. |
| 21. | Kinywa chake ni laini kuliko siagi, Bali moyo wake ni vita. Maneno yake ni mororo kuliko mafuta, Bali hayo ni panga wazi. |
| 22. | Umtwike Bwana mzigo wako naye atakutegemeza, Hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele. |
| 23. | Nawe, Ee Mungu, utawatelemsha, Walifikilie shimo la uharibifu; Watu wa damu na hila hawataishi nusu ya siku zao, Bali mimi nitakutumaini Wewe. |
| ← Psalms (55/150) → |