Psalms (51/150)  

1. Ee Mungu, unirehemu, Sawasawa na fadhili zako. Kiasi cha wingi wa rehema zako, Uyafute makosa yangu.
2. Unioshe kabisa na uovu wangu, Unitakase dhambi zangu.
3. Maana nimejua mimi makosa yangu Na dhambi yangu i mbele yangu daima.
4. Nimekutenda dhambi Wewe peke yako, Na kufanya maovu mbele za macho yako. Wewe ujulikane kuwa una haki unenapo, Na kuwa safi utoapo hukumu.
5. Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu; Mama yangu alinichukua mimba hatiani.
6. Tazama, wapendezwa na kweli iliyo moyoni; Nawe utanijulisha hekima kwa siri,
7. Unisafishe kwa hisopo nami nitakuwa safi, Unioshe, nami nitakuwa mweupe kuliko theluji
8. Unifanye kusikia furaha na shangwe, Mifupa uliyoiponda ifurahi.
9. Usitiri uso wako usitazame dhambi zangu; Uzifute hatia zangu zote.
10. Ee Mungu, uniumbie moyo safi, Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu
11. Usinitenge na uso wako, Wala roho yako mtakatifu usiniondolee.
12. Unirudishie furaha ya wokovu wako; Unitegemeze kwa roho ya wepesi.
13. Nitawafundisha wakosaji njia zako, Na wenye dhambi watarejea kwako.
14. Ee MUNGU, Mungu wa wokovu wangu, Uniponye na damu za watu, Na ulimi wangu utaiimba haki yako.
15. Ee Bwana, uifumbue midomo yangu, Na kinywa changu kitazinena sifa zako.
16. Maana hupendezwi na dhabihu, au ningeitoa, Wewe huridhii sadaka ya kuteketezwa.
17. Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika; Moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaudharau.
18. Uitendee mema Sayuni kwa radhi yako, Uzijenge kuta za Yerusalemu.
19. Ndipo utakapopendezwa na dhabihu za haki, Na sadaka za kuteketezwa, na kafara. Ndipo watakapotoa ng'ombe Juu ya madhabahu yako.

  Psalms (51/150)