| ← Proverbs (8/31) → |
| 1. | Je! Hekima halii? Ufahamu hatoi sauti yake? |
| 2. | Juu ya mahali palipoinuka karibu na njia, Penye njia panda, ndipo asimamapo. |
| 3. | Karibu na malango, mahali pa kuingia mjini, Mahali pa kuyaingilia malango anapiga kelele. |
| 4. | Enyi watu, nawaita ninyi; Na sauti yangu ni kwa wanadamu. |
| 5. | Enyi wajinga, fahamuni werevu, Nanyi wapumbavu, mpate moyo wa kufahamu. |
| 6. | Sikieni, maana nitasema yaliyo mazuri, Na kufumbua midomo yangu kutakuwa maadili. |
| 7. | Maana kinywa changu kitasema kweli, Na uovu ni chukizo kwa midomo yangu. |
| 8. | Maneno yote ya kinywa changu yana haki; Hapana hata neno lililopotoka au la ukaidi. |
| 9. | Yote humwelea yule afahamuye, Yote huelekea mbele yao waliopata maarifa. |
| 10. | Pokea mafundisho yangu, wala si fedha, Na maarifa kuliko dhahabu safi. |
| 11. | Maana hekima ni bora kuliko marijani; Wala vyote vinavyotamanika havilingani nayo. |
| 12. | Mimi, hekima, nimefanya werevu kuwa kao langu; Natafuta maarifa na busara. |
| 13. | Kumcha Bwana ni kuchukia uovu; Kiburi na majivuno, na njia mbovu, Na kinywa cha ukaidi pia nakichukia. |
| 14. | Shauri ni langu, na maarifa yaliyo sahihi; Mimi ni ufahamu, mimi nina nguvu. |
| 15. | Kwa msaada wangu wafalme humiliki, Na wakuu wanahukumu haki. |
| 16. | Kwa msaada wangu wakuu hutawala, Na waungwana, naam, waamuzi wote wa dunia. |
| 17. | Nawapenda wale wanipendao, Na wale wanitafutao kwa bidii wataniona. |
| 18. | Utajiri na heshima ziko kwangu, Naam, utajiri udumuo, na haki pia. |
| 19. | Matunda yangu hupita dhahabu, naam, dhahabu safi, Na faida yangu hupita fedha iliyo teule. |
| 20. | Natembea katika njia ya haki, Katikati ya mapito ya hukumu. |
| 21. | Niwarithishe mali wale wanipendao, Tena nipate kuzijaza hazina zao. |
| 22. | Bwana alikuwa nami katika mwanzo wa njia yake, Kabla ya matendo yake ya kale. |
| 23. | Nalitukuka tokea milele, tangu awali, Kabla haijawako dunia. |
| 24. | Wakati visipokuwako vilindi nalizaliwa, Wakati zisipokuwako chemchemi zilizojaa maji. |
| 25. | Kabla milima haijawekwa imara, Kabla ya vilima nalizaliwa. |
| 26. | Alipokuwa hajaiumba dunia, wala makonde Wala chanzo cha mavumbi ya dunia; |
| 27. | Alipozithibitisha mbingu nalikuwako; Alipopiga duara katika uso wa bahari; |
| 28. | Alipofanya imara mawingu yaliyo juu; Chemchemi za bahari zilipopata nguvu; |
| 29. | Alipoipa bahari mpaka wake, Kwamba maji yake yasiasi amri yake; Alipoiagiza misingi ya nchi; |
| 30. | Ndipo nilipokuwa pamoja naye, kama stadi wa kazi; Nikawa furaha yake kila siku; Nikifurahi daima mbele zake; |
| 31. | Nikiifurahia dunia inayokaliwa na watu; Na furaha yangu ilikuwa pamoja na wanadamu. |
| 32. | Basi, wanangu, nisikilizeni sasa; Maana heri hao wazishikao amri zangu. |
| 33. | Sikieni mafundisho, mpate hekima, Wala msiikatae. |
| 34. | Ana heri mtu yule anisikilizaye, Akisubiri sikuzote malangoni pangu, Akingoja penye vizingiti vya milango yangu. |
| 35. | Maana yeye anionaye mimi aona uzima, Naye atapata kibali kwa Bwana. |
| 36. | Bali anikosaye hujidhuru nafsi yake mwenyewe, Na wao wanichukiao hupenda mauti. |
| ← Proverbs (8/31) → |