| ← Proverbs (28/31) → |
| 1. | Waovu hukimbia wasipofuatiwa na mtu; Bali wenye haki ni wajasiri kama simba. |
| 2. | Kwa sababu ya maasi ya nchi wakuu wake huwa wengi; Bali kwa wenye ufahamu na maarifa hali ya nchi hudumishwa |
| 3. | Mtu mhitaji awaoneaye maskini, Ni kama mvua ya dhoruba isiyosaza chakula. |
| 4. | Wao waiachao sheria huwasifu waovu; Bali wao waishikao hushindana nao. |
| 5. | Watu wabaya hawaelewi na hukumu; Bali wamtafutao Bwana huelewa na yote. |
| 6. | Afadhali maskini aendaye katika unyofu wake, Kuliko mpotofu wa njia angawa ni tajiri. |
| 7. | Yeye aishikaye sheria ni mwana mwenye hekima; Bali aliye rafiki wa walafi humwaibisha babaye. |
| 8. | Yeye azidishaye mali yake kwa riba na faida, Humkusanyia mtu awahurumiaye maskini. |
| 9. | Yeye aligeuzaye sikio lake asiisikie sheria, Hata sala yake ni chukizo. |
| 10. | Kila mtu awapotezaye wenye haki katika njia mbaya, Ataanguka katika rima lake mwenyewe; Bali wakamilifu watarithi mema. |
| 11. | Mtu tajiri ana hekima machoni pake mwenyewe; Bali maskini mwenye ufahamu humchunguza sana. |
| 12. | Wenye haki washindapo, uko utukufu mwingi; Bali waovu waondokapo, watu hujificha. |
| 13. | Afichaye dhambi zake hatafanikiwa; Bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema. |
| 14. | Mwanadamu mwenye kicho yu heri sikuzote; Bali mshupavu wa moyo ataangukia madhara. |
| 15. | Kama simba angurumaye, na dubu mwenye njaa; Ndivyo alivyo mtu mbaya awatawalaye maskini. |
| 16. | Mkuu aliyepungukiwa na akili huwaonea watu sana; Bali achukiaye kutamani ataongeza siku zake. |
| 17. | Aliyelemewa na damu ya mtu Atalikimbilia shimo; wala mtu asimzuie. |
| 18. | Aendaye kwa unyofu ataokolewa; Bali mkaidi wa njia zake ataanguka mara. |
| 19. | Alimaye shamba lake atakuwa na chakula tele; Bali afuataye mambo ya upuzi atapata umaskini wa kumtosha. |
| 20. | Mtu mwaminifu atakuwa na baraka tele; Lakini afanyaye haraka kuwa tajiri hakosi ataadhibiwa. |
| 21. | Kupendelea watu si kwema; Wala mtu kuasi kwa ajili ya kipande cha mkate. |
| 22. | Mwenye husuda afanya haraka kuwa tajiri; Wala haufikiri uhitaji utakaomjilia. |
| 23. | Amkemeaye mwenzake hatimaye atapata kibali; Zaidi ya mtu ajipendekezaye kwa ulimi wake. |
| 24. | Aibaye mali ya babaye au mamaye, na kusema, Si kosa; Mwana huyo ni rafiki wa mtu mharibifu. |
| 25. | Mwenye nafsi ya kutamani huchochea fitina; Bali amtumainiye Bwana atawandishwa. |
| 26. | Mwenye kujitumainia moyo wake ni mjinga; Bali yeye aendaye kwa busara ataokolewa. |
| 27. | Mwenye kuwagawia maskini hatahitaji kitu; Bali afichaye macho yake atakuwa na laana nyingi. |
| 28. | Wasio haki wainukapo, wanadamu hujificha; Bali waangamiapo, wenye haki huongezeka. |
| ← Proverbs (28/31) → |