| ← Proverbs (2/31) → |
| 1. | Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, Na kuyaweka akiba maagizo yangu; |
| 2. | Hata ukatega sikio lako kusikia hekima, Ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; |
| 3. | Naam, ukiita busara, Na kupaza sauti yako upate ufahamu; |
| 4. | Ukiutafuta kama fedha, Na kuutafutia kama hazina iliyositirika; |
| 5. | Ndipo utakapofahamu kumcha Bwana, Na kupata kumjua Mungu. |
| 6. | Kwa kuwa Bwana huwapa watu hekima; Kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu; |
| 7. | Huwawekea wanyofu akiba ya hekima kamili; Yeye ni ngao kwao waendao kwa ukamilifu; |
| 8. | Apate kuyalinda mapito ya hukumu, Na kuhifadhi njia ya watakatifu wake. |
| 9. | Ndipo utakapofahamu haki na hukumu, Na adili, na kila njia njema. |
| 10. | Maana hekima itaingia moyoni mwako, Na maarifa yatakupendeza nafsi yako; |
| 11. | Busara itakulinda; Ufahamu utakuhifadhi. |
| 12. | Ili kukuokoa na njia ya uovu, Na watu wanenao yaliyopotoka; |
| 13. | Watu waziachao njia za unyofu, Ili kuziendea njia za giza; |
| 14. | Wafurahio kutenda mabaya; Wapendezwao na upotoe wa waovu; |
| 15. | Waliopotoka katika njia zao; Walio wakaidi katika mapito yao. |
| 16. | Ili kuokoka na malaya, Naam, malaya mwenye kubembeleza kwa maneno yake; |
| 17. | Amwachaye rafiki wa ujana wake, Na kulisahau agano la Mungu wake. |
| 18. | Maana nyumba yake inaelekea mauti, Na mapito yake yanakwenda kwenye wafu. |
| 19. | Katika hao wamwendeao harudi hata mmoja, Wala hawazifikilii njia za uzima. |
| 20. | Ili upate kwenda katika njia ya watu wema, Na kuyashika mapito ya wenye haki. |
| 21. | Maana wanyofu watakaa katika nchi, Na wakamilifu watadumu ndani yake. |
| 22. | Bali waovu watatengwa na nchi, Nao wafanyao hila watang'olewa. |
| ← Proverbs (2/31) → |