| ← Proverbs (18/31) → |
| 1. | Ajitengaye na wenzake hutafuta matakwa yake mwenyewe; Hushindana na kila shauri jema. |
| 2. | Mpumbavu hapendezwi na ufahamu; Ila moyo wake udhihirike tu. |
| 3. | Ajapo asiye haki, huja dharau pia; Na pamoja na aibu huja lawama. |
| 4. | Maneno ya kinywa cha mtu ni kama maji ya vilindi; Kijito kibubujikacho; chemchemi ya hekima. |
| 5. | Kukubali uso wake asiye haki si vizuri; Wala kumpotosha mwenye haki hukumuni. |
| 6. | Midomo ya mpumbavu huingia katika fitina, Na kinywa chake huita mapigo. |
| 7. | Kinywa cha mpumbavu ni uharibifu wake, Na midomo yake ni mtego wa nafsi yake. |
| 8. | Maneno ya mchongezi ni kama vitoweo; Nayo hushukia pande za ndani za tumbo. |
| 9. | Yeye naye aliye mvivu katika kazi yake, Ni ndugu yake aliye mharabu. |
| 10. | Jina la Bwana ni ngome imara; Mwenye haki huikimbilia, akawa salama. |
| 11. | Mali ya mtu tajiri ni mji wake wa nguvu; Ni kama ukuta mrefu katika mawazo yake. |
| 12. | Kabla ya uharibifu moyo wa mwanadamu hujivuna; Na kabla ya heshima hutangulia unyenyekevu. |
| 13. | Yeye ajibuye kabla hajasikia, Ni upumbavu na aibu kwake. |
| 14. | Roho ya mtu itastahimili udhaifu wake; Bali roho iliyovunjika nani awezaye kuistahimili? |
| 15. | Moyo wa mwenye busara hupata maarifa; Na sikio la mwenye hekima hutafuta maarifa. |
| 16. | Zawadi ya mtu humpatia nafasi; Humleta mbele ya watu wakuu. |
| 17. | Ajiteteaye kwanza huonekana kuwa ana haki; Lakini jirani yake huja na kumchunguza. |
| 18. | Kura hukomesha mashindano; Hukata maneno ya wakuu. |
| 19. | Ndugu aliyechukizwa ni mgumu kuliko mji wa nguvu; Na mashindano ni kama mapingo ya ngome. |
| 20. | Tumbo la mtu litajazwa matunda ya kinywa chake; Atashiba mazao ya midomo yake. |
| 21. | Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi; Na wao waupendao watakula matunda yake. |
| 22. | Apataye mke apata kitu chema; Naye ajipatia kibali kwa Bwana. |
| 23. | Maskini hutumia maombi; Bali tajiri hujibu kwa ukali. |
| 24. | Ajifanyiaye rafiki wengi ni kwa uangamivu wake mwenyewe; Lakini yuko rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu. |
| ← Proverbs (18/31) → |