| ← Proverbs (17/31) → |
| 1. | Afadhali mego kavu pamoja na utulivu, Kuliko nyumba yenye karamu nyingi pamoja na magomvi. |
| 2. | Mtumwa atendaye kwa busara atamtawala mwana atendaye mambo ya aibu; Tena atapata sehemu ya urithi kati ya ndugu. |
| 3. | Kalibuni kwa fedha, na tanuru kwa dhahabu; Bali Bwana huijaribu mioyo. |
| 4. | Mtenda mabaya husikiliza midomo ya uovu; Na mwongo hutega sikio lake kusikiliza ulimi wa madhara. |
| 5. | Amdhihakiye maskini humsuta Muumba wake; Naye aufurahiaye msiba hatakosa adhabu. |
| 6. | Wana wa wana ndio taji ya wazee, Na utukufu wa watoto ni baba zao. |
| 7. | Maneno mazuri hayapendezi kinywani mwa mpumbavu; Siuze midomo ya uongo kinywani mwa mkuu. |
| 8. | Kipawa ni kama kito cha thamani machoni pake yeye aliye nacho; Kila kigeukapo hufanikiwa. |
| 9. | Afunikaye kosa hutafuta kupendwa; Bali yeye akashifuye neno hutenga rafiki. |
| 10. | Lawama hupenya moyoni mwa mwenye ufahamu, Kuliko mapigo mia moyoni mwa mpumbavu. |
| 11. | Mtu mwovu hataki neno ila kuasi tu; Kwa hiyo mjumbe mkali atatumwa kwake. |
| 12. | Afadhali mtu akutwe na dubu aliyenyang'anywa watoto wake, Kuliko na mpumbavu katika upumbavu wake. |
| 13. | Yeye arudishaye mabaya badala ya mema, Mabaya hayataondoka nyumbani mwake. |
| 14. | Mwanzo wa ugomvi ni kama kutoboa penye maji; Basi acheni ugomvi kabla haujafurika. |
| 15. | Yeye asemaye kwamba asiye haki ana haki; naye asemaye kwamba mwenye haki hana haki; Hao wote wawili ni chukizo kwa Bwana. |
| 16. | Nini maana yake, mpumbavu kuwa na fedha mkononi mwake ya kununulia hekima, Ikiwa hana moyo wa ufahamu? |
| 17. | Rafiki hupenda sikuzote; Na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu. |
| 18. | Aliyepungukiwa na akili hupana mkono na mtu; Na kuwa mdhamini mbele ya mwenzake. |
| 19. | Apendaye ugomvi hupenda dhambi; Auinuaye sana mlango wake hutafuta uharibifu. |
| 20. | Mtu mwenye moyo wa ukaidi hatapata mema; Na mwenye ulimi wa upotofu huanguka katika misiba. |
| 21. | Azaaye mpumbavu ni kwa huzuni yake mwenyewe; Wala baba wa mpumbavu hana furaha. |
| 22. | Moyo uliochangamka ni dawa nzuri; Bali roho iliyopondeka huikausha mifupa. |
| 23. | Asiye haki hutoa rushwa kifuani, Ili kuzipotosha njia za hukumu. |
| 24. | Hekima huwa machoni pake mwenye ufahamu; Bali macho ya mpumbavu huwa katika ncha za dunia. |
| 25. | Mwana mpumbavu ni huzuni kwa babaye, Na uchungu kwa mamaye aliyemzaa. |
| 26. | Tena kumwadhibu mwenye haki si vizuri; Wala si kwema kuwapiga wakuu kwa unyofu wao. |
| 27. | Azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa; Na mwenye roho ya utulivu ana busara. |
| 28. | Hata mpumbavu akinyamaza, huhesabiwa hekima; Akifumba midomo yake, huhesabiwa ufahamu. |
| ← Proverbs (17/31) → |