| Proverbs (1/31) → | 
| 1. | Mithali za Sulemani, mwana wa Daudi, mfalme wa Israeli. | 
| 2. | Kujua hekima na adabu; kutambua maneno ya ufahamu; | 
| 3. | kufundishwa matendo ya busara, katika haki na hukumu na adili. | 
| 4. | Kuwapa wajinga werevu, na kijana maarifa na hadhari; | 
| 5. | mwenye hekima asikie na kuongezewa elimu, na mwenye ufahamu ayafikie mashauri yenye njia. | 
| 6. | Kufahamu mithali na kitendawili, na maneno ya wenye hekima na mafumbo yao. | 
| 7. | Kumcha Bwana ni chanzo cha maarifa, Bali wapumbavu hudharau hekima na adabu. | 
| 8. | Mwanangu, yasikilize mafundisho ya baba yako, Wala usiiache sheria ya mama yako, | 
| 9. | Kwa maana hayo yatakuwa kilemba cha neema kichwani pako, Na mikufu shingoni mwako. | 
| 10. | Mwanangu, wenye dhambi wakikushawishi, Wewe usikubali. | 
| 11. | Wakisema, Haya! Njoo pamoja nasi, Na tuvizie ili kumwaga damu; Tumwotee asiye na hatia, bila sababu; | 
| 12. | Tuwameze hai kama kuzimu, Na wazima, kama wao washukao shimoni. | 
| 13. | Tutapata mali yote ya thamani, Tutazijaza nyumba zetu mateka. | 
| 14. | Wewe utashirikiana nasi; Tutakuwa na vitu vyote shirika. | 
| 15. | Mwanangu, usiende njiani pamoja nao; Uzuie mguu wako usiende katika mapito yao. | 
| 16. | Maana miguu yao huenda mbio maovuni, Nao hufanya haraka ili kumwaga damu. | 
| 17. | Kwa kuwa mtego hutegwa bure, Mbele ya macho ya ndege ye yote. | 
| 18. | Na hao hujiotea damu yao wenyewe, Hujinyemelea nafsi zao wenyewe. | 
| 19. | Ndivyo zilivyo njia za kila mwenye tamaa ya mali; Huuondoa uhai wao walio nayo. | 
| 20. | Hekima hupaza sauti yake katika njia kuu, Hutoa sauti yake katika viwanja; | 
| 21. | Hulia penye mikutano mikubwa ya watu, Mahali pa kuyaingilia malango, Ndani ya mji hutamka maneno yake. | 
| 22. | Enyi wajinga, hata lini mtapenda ujinga? Na wenye dharau kupenda dharau yao, Na wapumbavu kuchukia maarifa? | 
| 23. | Geukeni kwa ajili ya maonyo yangu; Tazama, nitawamwagia roho yangu, Na kuwajulisheni maneno yangu. | 
| 24. | Kwa kuwa nimeita, nanyi mkakataa; Nimeunyosha mkono wangu, asiangalie mtu; | 
| 25. | Bali mmebatilisha shauri langu, Wala hamkutaka maonyo yangu; | 
| 26. | Mimi nami nitacheka siku ya msiba wenu, Nitadhihaki hofu yenu ifikapo; | 
| 27. | Hofu yenu ifikapo kama tufani, Na msiba wenu ufikapo kama kisulisuli, Dhiki na taabu zitakapowafikia. | 
| 28. | Ndipo watakaponiita, lakini sitaitika; Watanitafuta kwa bidii, wasinione. | 
| 29. | Kwa kuwa walichukia maarifa, Wala hawakuchagua kumcha Bwana. | 
| 30. | Hawakukubali mashauri yangu, Wakayadharau maonyo yangu yote. | 
| 31. | Kwa hiyo watakula matunda ya njia yao, Watashiba mashauri yao wenyewe. | 
| 32. | Maana kurudi nyuma kwao wajinga kutawaua, Na kufanikiwa kwao wapumbavu kutawaangamiza. | 
| 33. | Bali kila anisikilizaye atakaa salama, Naye atatulia bila kuogopa mabaya. | 
| Proverbs (1/31) → |