Numbers (4/36)  

1. Kisha Bwana akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia,
2. Katika wana wa Lawi uitenge hesabu ya wana wa Kohathi, kwa jamaa zao, na nyumba za baba zao,
3. tangu waliopata umri wa miaka thelathini na zaidi hata umri wa miaka hamsini, wote waingiao katika utumishi huo, ili kufanya kazi ya hema ya kukutania.
4. Huu ndio utumishi wa wana wa Kohathi katika hema ya kukutania, katika vile vyombo vitakatifu sana;
5. hapo watakapong'oa safari, Haruni ataingia ndani, na wanawe, nao watalishusha pazia la sitara, na kulifunika sanduku la ushahidi kwa hilo pazia;
6. kisha atatia juu yake ngozi za pomboo za kulifunikia, na kutandika juu yake nguo ya rangi ya samawi tupu, kisha watatia hiyo miti yake.
7. Tena juu ya meza ya mikate ya wonyesho watatandika nguo ya rangi ya samawi, na kuweka juu yake sahani, na miiko, na mabakuli, na vikombe vya kumiminia; na hiyo mikate ya daima itakuwa juu yake;
8. nao watatandika juu yake nguo ya rangi nyekundu, na kuifunika kwa ngozi za pomboo za kuifunikia, na kuitia ile miti yake.
9. Kisha watatwaa nguo ya rangi ya samawi, na kukifunika kinara cha taa ya nuru, na taa zake, na makasi yake, na sahani zake za kutilia makaa, na vyombo vyake vyote vya mafuta, watumiavyo kwa kazi yake;
10. nao watakitia, na vyombo vyake vyote, ndani ya ngozi ya pomboo, na kukitia juu ya miti ya kukichukulia
11. Tena watatandika nguo ya rangi ya samawi juu ya madhabahu ya dhahabu, na kuifunika kwa ngozi za pomboo, na kuitia ile miti yake;
12. kisha watavitwaa vile vyombo vyote vya utumishi wavitumiavyo katika mahali patakatifu, na kuvitia katika nguo ya rangi ya samawi, na kuvifunika kwa ngozi za pomboo, na kuvitia juu ya miti ya kuvichukulia.
13. Nao watayaondoa hayo majivu madhabahuni; na kutandika nguo ya rangi ya zambarau juu yake;
14. nao wataweka vyombo vyake vyote juu yake ambavyo wavitumia katika madhabahu, vyetezo, na nyuma, na miiko, na mabakuli, vyombo vyote vya hiyo madhabahu; nao watatandika juu yake ngozi za pomboo, na kutia miti yake mahali pake.
15. Na Haruni na wanawe watakapokwisha kupafunika mahali patakatifu, na vyombo vyote vya mahali patakatifu, hapo watakapong'oa kambi; baadaye, wana wa Kohathi watakuja kuvichukua; lakini wasiviguse vile vitu vitakatifu, wasife. Vyombo vile ni mzigo wa wana wa Kohathi katika hema ya kukutania.
16. Na ulinzi wake Eleazari mwana wa Haruni kuhani utakuwa ni kuyaangalia mafuta kwa nuru, na uvumba mzuri, na sadaka ya unga ya daima, na mafuta ya kupaka, tena ulinzi wa hiyo maskani yote, na wa vitu vyote vilivyo ndani yake, mahali patakatifu, na vyombo vyake.
17. Kisha Bwana akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia,
18. Msiitenge kabisa kabila ya jamaa za Wakohathi katika hao Walawi;
19. lakini wafanyieni neno hili, ili kwamba wawe hai, wasife, hapo watakapovikaribia vile vitu vilivyo vitakatifu sana; Haruni na wanawe wataingia ndani, na kuwawekea kila mtu utumishi wake, na kila mtu mzigo wake;
20. lakini wasiingie wao kupaona mahali pale patakatifu, hata kwa dakika moja, ili wasife.
21. Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia,
22. Fanya jumla ya wana wa Gershoni nao, kwa nyumba za baba zao, na jamaa zao;
23. tangu waliopata umri wa miaka thelathini na zaidi, hata umri wa miaka hamsini utawahesabu; wote watakaoingia kutumika, ili kufanya kazi katika hema ya kukutania.
24. Huu ni utumishi wa jamaa za Wagershoni, katika kutumika na katika kuchukua mizigo;
25. wao watayachukua mapazia ya maskani, na hema ya kukutania, hizo nguo za kufunikia, na zile ngozi za pomboo za kufunikia zilizo juu yake, na pazia la mlango wa hema ya kukutania;
26. na kuta za nguo za ua, na sitara ya ile nafasi ya kuingilia ya lango la ua, ulio karibu na maskani na madhabahu, kuzunguka pande zote, na kamba zake, na vyombo vyote vya utumishi wao, na yote yatakayotendeka kwavyo, watatumika katika hayo.
27. Utumishi wote wa wana wa Wagershoni, katika mzigo wao wote, na utumishi wao wote, utakuwa kwa amri ya Haruni na wanawe; nanyi mtawaagizia mzigo wao wote kuulinda.
28. Huu ni utumishi wa jamaa za wana wa Wagershoni katika hema kukutania; na ulinzi utakuwa chini ya mkono wa Ithamari mwana wa Haruni kuhani.
29. Katika habari ya wana wa Merari, utawahesabu kwa jamaa zao, na nyumba za baba zao;
30. tangu aliyepata umri wa miaka thelathini na zaidi, hata umri wa miaka hamsini, utawahesabu, kila atakayeingia katika huo utumishi, ili kufanya kazi ya hema ya kukutania.
31. Na mausia ya mzigo wao ni haya, kwa utumishi wao wote katika hema ya kukutania; mbao za maskani, na mataruma yake, na nguzo zake, na matako yake;
32. na viguzo vya ua vya kuuzunguka pande zote, na matako yake, na vigingi vyake, na kamba zake, na vyombo vyake vyote, pamoja na utumishi wake wote; nanyi mtawaagizia kila mtu kwa jina lake vile vyombo vya mzigo wao watakaoulinda.
33. Huu ni utumishi wa jamaa za wana wa Merari, kwa utumishi wao wote, katika hema ya kukutania, chini ya mkono wa Ithamari mwana wa Haruni kuhani.
34. Basi Musa na Haruni na hao wakuu wa mkutano wakawahesabu wana wa Kohathi kwa jamaa zao, na nyumba za baba zao,
35. tangu waliopata umri wa miaka thelathini na zaidi, hata umri wa miaka hamsini, kila mtu aliyeingia katika utumishi kwa kazi katika hema ya kukutania,
36. na waliohesabiwa kwao kwa jamaa zao, walikuwa elfu mbili na mia saba hamsini.
37. Hao ndio waliohesabiwa katika jamaa za Wakohathi, wote waliotumika katika hema ya kukutania, ambao Musa na Haruni waliwahesabu kwa amri ya Bwana kwa mkono wa Musa.
38. Na hao waliohesabiwa katika wana wa Gershoni, kwa jamaa zao na nyumba zao baba zao,
39. tangu waliopata umri wa miaka thelathini na zaidi, hata umri wa miaka hamsini, kila mtu aliyeingia katika utumishi, kwa kazi katika hema ya kukutania,
40. hata wale waliohesabiwa kwao, kwa jamaa zao na nyumba za baba zao, walikuwa elfu mbili na mia sita na thelathini.
41. Hao ndio waliohesabiwa katika jamaa za wana wa Gershoni, wote waliotumika katika hema ya kukutania, ambao Musa na Haruni waliwahesabu kwa amri ya Bwana.
42. Na hao waliohesabiwa katika jamaa za wana wa Merari, kwa jamaa zao, na nyumba za baba zao,
43. tangu waliopata umri wa miaka thelathini na zaidi, hata umri wa miaka hamsini, kila mtu aliyeingia katika utumishi kwa kazi katika hema ya kukutania,
44. wale waliohesabiwa kwao, kwa jamaa zao, walikuwa elfu tatu na mia mbili.
45. Hao ndio waliohesabiwa katika jamaa za wana wa Merari, ambao Musa na; Haruni waliwahesabu kwa amri ya Bwana, kwa mkono wa Musa.
46. Wote waliohesabiwa katika Walawi, ambao Musa na Haruni na hao wakuu wa Israeli waliwahesabu, kwa jamaa zao, na nyumba za baba zao,
47. tangu waliopata umri wa miaka thelathini na zaidi, hata umri wa miaka hamsini, kila aliyeingia kufanya kazi ya utumishi, na kazi ya kuchukua mizigo katika hema ya kukutania,
48. hao waliohesabiwa kwao, walikuwa elfu nane na mia tano themanini.
49. Kwa amri ya Bwana, walihesabiwa kwa mkono wa Musa, kila mtu kwa utumishi wake, na kama mzigo wake ulivyokuwa; ndivyo walivyohesabiwa na yeye, kama Bwana alivyomwagiza Musa.

  Numbers (4/36)