Micah (2/7)  

1. Ole wao wakusudiao mambo maovu, na kutenda mabaya vitandani mwao! Kunapopambazuka asubuhi huyafanya, kwa sababu ya katika uwezo wa mikono yao.
2. Nao hutamani mashamba, na kuyashika; na nyumba pia, nao huzichukua; nao humwonea mtu na nyumba yake, naam, mtu na urithi wake.
3. Basi Bwana asema hivi, Angalia, nakusudia jambo baya juu ya jamaa hii, ambalo hamtazitoa shingo zenu, wala hamtakwenda kwa kiburi; kwa maana ni wakati mbaya.
4. Siku hiyo watatunga mithali juu yenu, na kuomboleza kwa maombolezo ya huzuni nyingi, na kusema, Sisi tumeangamizwa kabisa; Yeye analibadili fungu la watu wangu; Jinsi anavyoniondolea hilo! Awagawia waasi mashamba yetu.
5. Kwa hiyo hutakuwa na mtu atakayeitupa kamba kwa kura katika mkutano wa Bwana.
6. Msitabiri, ndivyo watabirivyo; wasiyatabiri mambo haya; lawama hazikomi.
7. Je! Litasemwa neno hili, enyi nyumba ya Yakobo, Roho ya Bwana imepunguzwa? Je! Haya ni matendo yake? Je! Maneno yangu hayamfai yeye aendaye kwa unyofu?
8. Lakini siku hizi mmeinuka kama adui za watu wangu; mwaipokonya joho iliyo juu ya nguo za hao wapitao salama kama watu wasiopenda vita.
9. Wanawake wa watu wangu mwawatupa nje ya nyumba zao nzuri; watoto wao wachanga mwawanyang'anya utukufu wangu milele.
10. Ondokeni, mwende zenu; maana hapa sipo mahali pa raha yenu; kwa sababu ya uchafu mtaangamizwa, naam, kwa maangamizo mazito sana.
11. Mtu akienda kwa roho ya uongo, akinena maneno ya uongo, akisema, Nitakutabiria habari ya mvinyo na kileo; mtu huyu atakuwa nabii wao watu hawa.
12. Hakika nitakukusanya, Ee Yakobo, nyote pia; Bila shaka nitawakusanya waliobaki wa Israeli; Nitawaweka pamoja kama kondoo wa Bozra; Kama kundi la kondoo kati ya malisho yao; Watafanya mvumo kwa wingi wa watu;
13. Avunjaye amekwea juu mbele yao; Wamebomoa mahali, wakapita mpaka langoni, Wakatoka nje huko; Mfalme wao naye amepita akiwatangulia, Naye Bwana ametangulia mbele yao.

  Micah (2/7)