Leviticus (27/27)    

1. Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia,
2. Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Hapo mtu atakapoondoa nadhiri, hizo nafsi za watu zitakuwa kwa Bwana, kama utakavyowahesabia wewe.
3. Na hesabu yako itakuwa kwa mtu mume, tokea aliye na umri wa miaka ishirini hata umri wa miaka sitini, hesabu yako itakuwa shekeli hamsini za fedha, kwa shekeli ya mahali patakatifu.
4. Kama ni mwanamke, hesabu yako itakuwa shekeli thelathini.
5. Tena akiwa mwenye umri wa miaka mitano hata umri wa miaka ishirini, ndipo hesabu yako itakuwa shekeli ishirini kwa mwanamume, na shekeli kumi kwa mwanamke.
6. Tena akiwa mwenye umri wa mwezi mmoja hata umri wa miaka mitano, ndipo hesabu yako itakuwa shekeli tano za fedha kwa mwanamume, na hesabu yako itakuwa shekeli tatu za fedha kwa mwanamke.
7. Tena akiwa mwenye umri wa miaka sitini na kuzidi; kama ni mwanamume, hesabu yako itakuwa shekeli kumi na tano, na kwa mwanamke shekeli kumi.
8. Lakini kwamba ni maskini zaidi ya kuhesabu kwako, ndipo atawekwa mbele ya kuhani, na huyo kuhani atamtia kima; kama uwezo wake huyo aliyeweka nadhiri ulivyo, ndivyo kuhani atakavyomtia kima.
9. Tena kama ni mnyama wa namna ambayo watu husongeza kuwa sadaka kwa Bwana, kila mmoja katika wanyama hao atakayetolewa kwa Bwana, na mtu ye yote, atakuwa ni mtakatifu.
10. Yeye hatamgeuza, wala kumbadili mwema kwa mbaya, au mbaya kwa mwema; kwamba atabadili mnyama kwa mnyama ye yote, ndipo mnyama huyo na yule waliobadiliwa wote wawili watakuwa watakatifu.
11. Na kama ni mnyama ye yote asiye safi, wa namna ambayo hawamsongezi kwa Bwana, basi atamweka huyo mnyama mbele ya kuhani;
12. na kuhani atamtia kima, akiwa mwema akiwa mbaya; kama wewe kuhani utakavyomtia kima, ndivyo itakavyokuwa.
13. Lakini kwamba ataka kumkomboa kweli, ndipo atakapoongeza sehemu ya tano juu ya hesabu yako.
14. Na mtu atakapoiweka nyumba yake iwe wakfu kwa Bwana ndipo kuhani ataihesabu kima chake hiyo nyumba, ikiwa njema ikiwa mbaya; kama kuhani atakavyoihesabu kima chake ndivyo itakavyokuwa.
15. Tena mtu huyo aliyeweka nyumba yake iwe wakfu kama akitaka kuikomboa, ndipo atakapoongeza sehemu ya tano ya hiyo fedha ya hesabu yako, nayo itakuwa mali yake.
16. Tena kama mtu akiweka wakfu kwa Bwana sehemu ya shamba la milki yake, ndipo hesabu yako itakuwa kama kule kupanda kwake kulivyo; kupanda kwake homeri moja ya mbegu ya shayiri, kutahesabiwa kuwa ni shekeli hamsini za fedha.
17. Kwamba anaweka shamba lake liwe wakfu tangu mwaka wa yubile, litasimama vivyo kama hesabu yako ilivyo.
18. Lakini akiliweka shamba lake wakfu baada ya yubile, ndipo kuhani atamhesabia hiyo fedha kama hesabu ya miaka iliyobaki hata mwaka wa yubile, na kuhesabiwa kwako kutapunguzwa.
19. Na kama yeye aliyeliweka shamba wakfu akitaka kulikomboa kweli, ndipo atakapoongeza sehemu ya tano ya hiyo fedha ya hesabu yako, nalo litathibitishwa kwake.
20. Lakini asipotaka kulikomboa shamba, au kama amemwuzia mtu mwingine hilo shamba, halitakombolewa tena kabisa;
21. ila hilo shamba litakuwa takatifu kwa Bwana litakapotoka katika yubile, kama ni shamba lililowekwa wakfu; litakuwa mali ya kuhani.
22. Tena kama akiweka wakfu kwa Bwana shamba ambalo amelinunua, ambalo si shamba la milki yake;
23. ndipo kuhani atamhesabia kima cha kuhesabu kwako hata mwaka wa yubile: naye atatoa siku hiyo kama hesabu yako, kuwa ni kitu kitakatifu kwa Bwana.
24. Mwaka wa yubile shamba hilo litarejea kwake huyo ambaye lilinunuliwa kwake, yaani, huyo ambaye nchi hiyo ni milki yake.
25. Na hesabu zako zote zitaandamana shekeli ya mahali patakatifu; gera ishirini zitakuwa shekeli moja.
26. Mzaliwa wa kwanza tu katika wanyama, aliyewekwa kuwa mzaliwa wa kwanza kwa Bwana, mtu awaye yote hatamweka kuwa mtakatifu; kama ni ng'ombe, kama ni kondoo, huyo ni wa Bwana.
27. Na kama ni wa mnyama asiye safi, ndipo atamkomboa kama hesabu yako ilivyo, naye ataongeza sehemu ya tano ya bei yake; au asipokombolewa, ndipo atauzwa kama hesabu yako ilivyo.
28. Pamoja na hayo, hakitauzwa wala kukombolewa kitu cho chote kilichowekwa wakfu, ambacho mtu amekiweka wakfu kwa Bwana, katika vitu vyote alivyo navyo, kama ni mtu, au mnyama, au kama ni shamba la milki yake; kila kitu kilichowekwa wakfu ni kitakatifu sana kwa Bwana.
29. Kila aliyewekwa wakfu, aliyewekwa wakfu na binadamu, hatakombolewa; sharti atauawa.
30. Tena zaka yote ya nchi, kama ni mbegu ya nchi, au kama ni matunda ya nchi, ni ya Bwana; ni takatifu kwa Bwana.
31. Na kama mtu akitaka kukomboa cho chote cha zaka yake, ataongeza sehemu yake ya tano juu yake.
32. Tena zaka yote ya ng'ombe, au ya kondoo, kila apitaye chini ya fimbo; sehemu ya kumi watakuwa ni watakatifu kwa Bwana.
33. Hataangalia kwamba ni mwema au kwamba ni mbaya, wala hatambadili; na kama akimbadili na yo yote, ndipo wote wawili, huyo na huyo waliobadiliwa watakuwa ni watakatifu; hatakombolewa.
34. Haya ndiyo maagizo, Bwana aliyomwagiza Musa kwa ajili ya wana wa Israeli katika mlima wa Sinai.

  Leviticus (27/27)