| ← John (4/21) → |
| 1. | Kwa hiyo Bwana, alipofahamu ya kuwa Mafarisayo wamesikia ya kwamba, Yesu anafanya wanafunzi wengi kuliko Yohana, na kuwabatiza, |
| 2. | (lakini Yesu mwenyewe hakubatiza, bali wanafunzi wake,) |
| 3. | aliacha Uyahudi, akaenda zake tena mpaka Galilaya. |
| 4. | Naye alikuwa hana budi kupita katikati ya Samaria. |
| 5. | Basi akafika kunako mji wa Samaria, uitwao Sikari, karibu na lile shamba ambalo Yakobo alimpa Yusufu mwanawe. |
| 6. | Na hapo palikuwa na kisima cha Yakobo. Basi Yesu, kwa sababu amechoka kwa safari yake, akaketi vivi hivi kisimani. Nayo ilikuwa yapata saa sita. |
| 7. | Akaja mwanamke Msamaria kuteka maji. Yesu akamwambia, Nipe maji ninywe. |
| 8. | Kwa maana wanafunzi wake wamekwenda mjini kununua chakula. |
| 9. | Basi yule mwanamke Msamaria akamwambia, Imekuwaje wewe Myahudi kutaka maji kwangu, nami ni mwanamke Msamaria? (Maana Wayahudi hawachangamani na Wasamaria.) |
| 10. | Yesu akajibu, akamwambia, Kama ungaliijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, Nipe maji ninywe, ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai. |
| 11. | Yule mwanamke akamwambia, Bwana, huna kitu cha kutekea, na kisima ni kirefu; basi umeyapata wapi hayo maji yaliyo hai? |
| 12. | Je! Wewe u mkubwa kuliko baba yetu, Yakobo, aliyetupa kisima hiki, naye mwenyewe akanywa maji yake, na wanawe pia, na wanyama wake? |
| 13. | Yesu akajibu, akamwambia, Kila anywaye maji haya ataona kiu tena; |
| 14. | walakini ye yote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele. |
| 15. | Yule mwanamke akamwambia, Bwana, unipe maji hayo, nisione kiu, wala nisije hapa kuteka. |
| 16. | Yesu akamwambia, Nenda kamwite mumeo, uje naye hapa. |
| 17. | Yule mwanamke akajibu, akasema, Sina mume. Yesu akamwambia, Umesema vema, Sina mume; |
| 18. | kwa maana umekuwa na waume watano, naye uliye naye sasa siye mume wako; hapo umesema kweli. |
| 19. | Yule mwanamke akamwambia, Bwana, naona ya kuwa u nabii! |
| 20. | Baba zetu waliabudu katika mlima huu, nanyi husema ya kwamba huko Yerusalemu ni mahali patupasapo kuabudia. |
| 21. | Yesu akamwambia, Mama, unisadiki, saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu, wala kule Yerusalemu. |
| 22. | Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tukijuacho; kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi. |
| 23. | Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. |
| 24. | Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli. |
| 25. | Yule mwanamke akamwambia, Najua ya kuwa yuaja Masihi, (aitwaye Kristo); naye atakapokuja, yeye atatufunulia mambo yote. |
| 26. | Yesu akamwambia, Mimi ninayesema nawe, ndiye. |
| 27. | Mara hiyo wakaja wanafunzi wake, wakastaajabu kwa sababu alikuwa akisema na mwanamke; lakini hakuna aliyesema, Unatafuta nini? Au, Mbona unasema naye? |
| 28. | Basi yule mwanamke akauacha mtungi wake, akaenda zake mjini, akawaambia watu, |
| 29. | Njoni, mtazame mtu aliyeniambia mambo yote niliyoyatenda. Je! Haimkini huyu kuwa ndiye Kristo? |
| 30. | Basi wakatoka mjini, wakamwendea. |
| 31. | Huko nyuma wanafunzi wakamsihi wakisema, Rabi, ule. |
| 32. | Akawaambia, Mimi ninacho chakula msichokijua ninyi. |
| 33. | Basi wanafunzi wake wakasemezana, Je! Mtu amemletea chakula? |
| 34. | Yesu akawaambia, Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake. |
| 35. | Hamsemi ninyi, Bado miezi minne, ndipo yaja mavuno? Tazama, mimi nawaambieni, Inueni macho yenu myatazame mashamba, ya kuwa yamekwisha kuwa meupe, tayari kwa mavuno. |
| 36. | Naye avunaye hupokea mshahara, na kukusanya matunda kwa uzima wa milele, ili yeye apandaye na yeye avunaye wapate kufurahi pamoja. |
| 37. | Kwa maana hapo neno hilo huwa kweli, Mmoja hupanda akavuna mwingine. |
| 38. | Mimi naliwatuma myavune yale msiyoyataabikia; wengine walitaabika, nanyi mmeingia katika taabu yao. |
| 39. | Na katika mji ule Wasamaria wengi walimwamini kwa sababu ya neno la yule mwanamke, aliyeshuhudia kwamba, Aliniambia mambo yote niliyoyatenda. |
| 40. | Basi wale Wasamaria walipomwendea, walimsihi akae kwao; naye akakaa huko siku mbili. |
| 41. | Watu wengi zaidi wakaamini kwa sababu ya neno lake. |
| 42. | Wakamwambia yule mwanamke, Sasa tunaamini, wala si kwa sababu ya maneno yako tu; maana sisi tumesikia wenyewe, tena twajua ya kuwa hakika huyu ndiye Mwokozi wa ulimwengu. |
| 43. | Na baada ya siku mbili hizo akaondoka huko, akaenda Galilaya. |
| 44. | Kwa maana Yesu mwenyewe alishuhudia ya kwamba nabii hapati heshima katika nchi yake mwenyewe. |
| 45. | Basi alipotoka Galilaya, Wagalilaya walimpokea; kwa kuwa wameyaona mambo yote aliyoyatenda huko Yerusalemu wakati wa sikukuu; maana hao nao waliiendea sikukuu. |
| 46. | Basi alifika tena Kana ya Galilaya, hapo alipoyafanya yale maji kuwa divai. Na palikuwa na diwani mmoja ambaye mwanawe hawezi huko Kapernaumu. |
| 47. | Huyo aliposikia ya kwamba Yesu amekuja kutoka Uyahudi mpaka Galilaya, alimwendea, akamsihi ashuke na kumponya mwanawe; kwa maana alikuwa kufani. |
| 48. | Basi Yesu akamwambia, Msipoona ishara na maajabu hamtaamini kabisa? |
| 49. | Yule diwani akamwambia, Bwana, ushuke asijakufa mtoto wangu. |
| 50. | Yesu akamwambia, Enenda; mwanao yu hai. Mtu yule akalisadiki lile neno aliloambiwa na Yesu, naye akashika njia. |
| 51. | Hata alipokuwa akishuka, watumwa wake walimlaki, wakisema ya kwamba mtoto wake yu hai. |
| 52. | Basi akawauliza habari ya saa alipoanza kuwa hajambo; nao wakamwambia, Jana, saa saba, homa ilimwacha. |
| 53. | Basi babaye akafahamu ya kuwa ni saa ile ile aliyoambiwa na Yesu, Mwanao yu hai. Akaamini yeye na wote wa nyumbani mwake. |
| 54. | Hiyo ni ishara ya pili aliyoifanya Yesu, alipokuwa ametoka Uyahudi kufika Galilaya. |
| ← John (4/21) → |