← Job (9/42) → |
1. | Ndipo Ayubu akajibu, na kusema, |
2. | Kweli najua kuwa ndivyo hivyo; Lakini mtu huwaje mwenye haki mbele za Mungu? |
3. | Kama akipenda kushindana naye, Hawezi kumjibu neno moja katika elfu. |
4. | Yeye ni mwenye hekima moyoni, na mwenye uwezo katika nguvu; Ni nani aliyejifanya kuwa mgumu juu yake, naye akafanikiwa? |
5. | Aiondoaye milima, nayo haina habari, Akiipindua katika hasira zake. |
6. | Aitikisaye dunia itoke mahali pake, Na nguzo zake hutetema. |
7. | Aliamuruye jua, nalo halichomozi; Nazo nyota huzipiga muhuri. |
8. | Ambaye peke yake ni mwenye kuzitandika mbingu, Na kuyakanyaga mawimbi ya bahari. |
9. | Yeye afanyaye hizo nyota za Dubu, na Orioni, na hicho Kilimia, Na makundi ya nyota ya kusini. |
10. | Atendaye mambo makuu yasiyotafutikana; Naam, mambo ya ajabu yasiyohesabika. |
11. | Tazama, yuaenenda karibu nami, nisimwone; Tena yuapita kwenda mbele, nisimtambue. |
12. | Tazama, yuakamata, ni nani awezaye kumzuia? Ni nani awezaye kumwuliza, Wafanya nini? |
13. | Mungu haondoi hasira zake; Hao wamsaidiao Rahabu huinama chini yake. |
14. | Je! Mimi nitamjibuje, Na kuyachagua maneno yangu kuhojiana naye? |
15. | Ambaye, nijapokuwa mimi ni mwenye haki, nisingemjibu; Ningemsihi-sihi mtesi wangu. |
16. | Kama ningemwita, naye akaniitikia; Hata hivyo singeamini kuwa amesikiza sauti yangu. |
17. | Yeye anipondaye kwa dhoruba, Na kuziongeza jeraha zangu pasipokuwa na sababu. |
18. | Haniachi nipate kuvuta pumzi, Lakini hunijaza uchungu. |
19. | Kama tukitaja nguvu za mashujaa, tazama yupo hapo! Kama tukitaja hukumu, ni nani atakayeniwekea muhula? |
20. | Ingawa ni mwenye haki, kinywa changu mwenyewe kitanihukumu; Ingawa ni mkamilifu, kitanishuhudia kuwa ni mpotovu. |
21. | Mimi ni mkamilifu; siangalii nafsi yangu; Naudharau uhai wangu. |
22. | Hayo yote ni mamoja; kwa hiyo nasema, Yeye huangamiza wakamilifu na waovu pia. |
23. | Kama hilo pigo likiua ghafula, Atayadhihaki majaribu yake asiye na kosa. |
24. | Dunia imetiwa mkononi mwa waovu; Yeye hufunika nyuso za waamuzi wake; Kama si yeye, ni nani basi? |
25. | Basi siku zangu zina mbio kuliko tarishi; Zakimbia, wala hazioni mema. |
26. | Zimepita kama merikebu ziendazo mbio; Mfano wa tai ayashukiaye mawindo. |
27. | Nikisema, Mimi nitasahau kuugua kwangu, Nitaacha kununa uso nikachangamke moyo; |
28. | Mimi huziogopa huzuni zangu zote, Najua kuwa hutanihesabu kuwa sina hatia. |
29. | Nitahukumiwa kuwa ni mkosa; Ya nini basi nitaabike bure? |
30. | Ingawaje najiosha kwa maji ya theluji, Na kuitakasa mikono yangu kwa sabuni; |
31. | Lakini utanitupa shimoni, Nami hata nguo zangu zitanichukia. |
32. | Kwani yeye si mtu, kama mimi, hata nimjibu, Hata tukaribiane katika hukumu. |
33. | Hapana mwenye kuamua katikati yetu, Awezaye kutuwekea mkono sote wawili. |
34. | Na aniondolee fimbo yake, Na utisho wake usinitie hofu; |
35. | Ndipo hapo ningesema, nisimwogope; Kwani sivyo nilivyo nafsini mwangu. |
← Job (9/42) → |