← Job (4/42) → |
1. | Ndipo huyo Elifazi, Mtemani, akajibu na kusema, |
2. | Mtu akijaribu kuzungumza nawe, je! Utaona ni vibaya? Lakini ni nani awezaye kujizuia asinene? |
3. | Tazama, wewe umewafunza watu wengi, Nawe umeitia nguvu mikono iliyokuwa minyonge. |
4. | Maneno yako yamemtegemeza huyo aliyekuwa anaanguka, Nawe umeyaimarisha magoti manyonge. |
5. | Lakini sasa haya yamekufikilia wewe, nawe wafa moyo; Yamekugusa, nawe wafadhaika. |
6. | Je! Dini yako siyo mataraja yako, Na matumaini yako si huo uelekevu wa njia zako? |
7. | Kumbuka, tafadhali, ni nani aliyeangamia akiwa hana hatia? Au hao waelekevu, walikatiliwa mbali wapi? |
8. | Kama mimi nilivyoona, hao walimao maovu, Na kupanda madhara, huvuna yayo hayo. |
9. | Kwa pumzi za Mungu huangamia. Na kwa kuvuma kwa hasira zake humalizika. |
10. | Kunguruma kwake simba, na sauti ya simba mkali, Na meno ya simba wachanga, yamevunjika. |
11. | Simba mzee huangamia kwa kukosa mawindo, Nao watoto wa simba mke wametawanyika mbalimbali. |
12. | Basi, nililetewa neno kwa siri, Sikio langu likasikia manong'ono yake. |
13. | Katika mawazo yaliyotoka katika maono ya usiku, Hapo usingizi mzito uwaangukiapo wanadamu. |
14. | Hofu iliniangukia na kutetema, Iliyoitetemesha mifupa yangu yote. |
15. | Ndipo pepo ilipita mbele ya uso wangu; Na nywele za mwili wangu zilisimama. |
16. | Hiyo pepo ilisimama kimya, nisiweze kutambua sura zake, Mfano ulikuwa mbele ya macho yangu; Kulikuwa kimya, nami nilisikia sauti, ikinena, |
17. | Je! Binadamu atakuwa na haki kuliko Mungu? Je! Mtu atakuwa safi kuliko Muumba wake? |
18. | Tazama, yeye hawategemei watumishi wake; Na malaika zake huwahesabia upuzi; |
19. | Je! Si zaidi sana hao wakaao katika nyumba za udongo, Ambazo misingi yao i katika mchanga, Hao waliosetwa mbele ya nondo! |
20. | Kati ya asubuhi na jioni huvunjwa-vunjwa; Waangamia milele wala hapana atiaye moyoni. |
21. | Je! Kamba ya hema yao haikung'olewa ndani yao? Wafa, kisha hali hawana akili. |
← Job (4/42) → |