| ← Job (28/42) → |
| 1. | Hakika kuna shimo wachimbako fedha, Na mahali wapatapo dhahabu waisafishayo. |
| 2. | Chuma hufukuliwa katika ardhi, Na shaba huyeyushwa katika mawe. |
| 3. | Binadamu hukomesha giza; Huyatafuta-tafuta hata mpaka ulio mbali, Mawe ya giza kuu, giza tupu. |
| 4. | Hufukua shimo mbali na makao ya watu; Husahauliwa na nyayo zipitazo; Huning'inia mbali na watu, huyumba-yumba huko na huko. |
| 5. | Katika ardhi ndimo kitokeamo chakula; Na chini yake hupinduliwa kama kwa moto. |
| 6. | Mawe yake ni mahali zipatikanapo yakuti; Nayo ina mchanga wa dhahabu. |
| 7. | Njia ile hapana ndege mkali aijuaye, Wala jicho la tai halijaiona; |
| 8. | Wanyama wakali wajivunao hawajaikanyaga, Wala simba mkali hajaipita. |
| 9. | Huunyoshea mwamba wa gumegume mkono wake; Huipindua milima hata misingi yake. |
| 10. | Hukata mifereji kati ya majabali; Na jicho lake huona kila kito cha thamani |
| 11. | Hufunga vijito visichuruzike; Na kitu kilichostirika hukifunua. |
| 12. | Bali hekima itapatikana wapi? Na mahali pa ufahamu ni wapi? |
| 13. | Mwanadamu hajui thamani yake, Wala haionekani katika nchi ya walio hai. |
| 14. | Vilindi vyasema, Haimo ndani yangu; Na bahari yasema, Haiko kwangu. |
| 15. | Haipatikani kwa dhahabu, Wala fedha haitapimwa iwe thamani yake. |
| 16. | Haiwezi kutiwa thamani kwa dhahabu ya Ofiri, Wala kwa shohamu ya thamani nyingi, wala kwa yakuti ya samawi. |
| 17. | Dhahabu na vioo haviwezi kulinganishwa nayo; Wala kubadili kwake hakutakuwa kwa vyombo vya dhahabu safi. |
| 18. | Havitatajwa fedhaluka wala bilauri; Naam, kima cha hekima chapita marijani. |
| 19. | Yakuti ya rangi ya manjano ya Kushi haitasawazishwa nayo, Wala haitatiwa kima kwa dhahabu safi. |
| 20. | Basi hekima yatoka wapi? Na mahali pa ufahamu ni wapi? |
| 21. | Kwa kuwa imefichwa mbali na macho ya wote walio hai, Na kusitirika na ndege wa angani. |
| 22. | Uharibifu na Mauti husema, Tumesikia habari zake kwa masikio yetu. |
| 23. | Mungu ndiye aijuaye njia yake, Naye anajua mahali pake. |
| 24. | Maana anatazama hata miisho ya nchi, Na kuona chini ya mbingu nzima. |
| 25. | Apate kuufanyia upepo uzito wake; Naam, anayapima maji kwa kipimo. |
| 26. | Hapo alipoiwekea mvua amri, Na njia kwa umeme wa radi. |
| 27. | Ndipo alipoiona na kuitangaza; Aliithibitisha, naam, na kuichunguza. |
| 28. | Kisha akamwambia mwanadamu, Tazama, kumcha Bwana ndiyo hekima, Na kujitenga na uovu ndio ufahamu. |
| ← Job (28/42) → |