← Jeremiah (48/52) → |
1. | Habari za Moabu. Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Ole wake Nebo! Kwa maana umeharibika; Kiriathaimu umeaibishwa, umetwaliwa; Misgabu umeaibishwa, nao umebomolewa. |
2. | Sifa za Moabu haziko tena; katika Heshboni wameazimia mabaya juu yake, Haya! Njoni, na tumkatilie mbali asiwe taifa. Wewe nawe, Ee Madmena, utanyamazishwa; upanga utakufuatia. |
3. | Sauti ya kilio toka Horonaimu, Ya kutekwa na uharibifu mkuu. |
4. | Moabu umeharibika; Wadogo wake wamewasikiza watu kilio. |
5. | Kwa maana watu wapandapo huko Luhithi Watapanda wasiache kulia; Nao watu watelemkapo huko Horonaimu Wameisikia huzuni ya kilio cha uharibifu. |
6. | Haya! Kimbieni! Jiokoeni nafsi zenu! Mkawe kama mtu aliye mkiwa. |
7. | Maana, kwa kuwa umeyatumainia matendo yako, na hazina zako, wewe nawe utatwaliwa; na Kemoshi atatoka aende katika uhamisho, makuhani wake na wakuu wake pamoja. |
8. | Naye mwenye kuteka nyara atakuja juu ya kila mji, wala hapana mji utakaookoka; bonde nalo litaangamia, nayo nchi tambarare itaharibiwa; kama Bwana alivyosema. |
9. | Mpe Moabu mabawa, apate kuruka na kwenda zake; na miji yake itakuwa ukiwa, isiwe na mtu wa kukaa ndani yake. |
10. | Na alaaniwe mtu afanyaye kazi ya Bwana kwa ulegevu; na alaaniwe auzuiaye upanga wake usimwage damu. |
11. | Moabu amestarehe tangu ujana wake, naye ametulia juu ya sira zake, wala hakumiminwa kutoka chombo kimoja kutiwa chombo kingine, wala hakwenda kufungwa; kwa hiyo ladha yake anakaa nayo, wala harufu yake haikubadilika. |
12. | Basi, tazama, siku zinakuja, asema Bwana, ambazo nitampelekea wamiminao, nao watammimina, nao watamwaga vyote vilivyomo vyomboni mwake, na kuzivunja chupa zake vipande vipande. |
13. | Na Moabu ataona haya kwa ajili ya Kemoshi, kama nyumba ya Israeli ilivyoona haya kwa ajili ya Betheli, matumaini yao. |
14. | Mwasemaje ninyi, Sisi tu mashujaa, watu hodari wa vita. |
15. | Moabu ameharibika, na moshi wa miji yake umepanda; na vijana wake wateule wametelemka kwenda kuchinjwa, asema Mfalme, ambaye jina lake ni Bwana wa majeshi. |
16. | Msiba wa Moabu umefika karibu, Na mateso yake yanafanya haraka. |
17. | Ninyi nyote mnaomzunguka, mlilieni, Nanyi nyote mlijuao jina lake, semeni, Jinsi ilivyovunjika fimbo ya enzi, Fimbo ile iliyokuwa nzuri! |
18. | Ee binti ukaaye Diboni, Shuka toka utukufu wako, ukae katika kiu; Maana atekaye Moabu amepanda juu yako, Ameziharibu ngome zako. |
19. | Wewe ukaaye Aroeri, Simama kando ya njia upeleleze; Mwulize mwanamume akimbiaye na mwanamke atorokaye, Sema, Imetendeka nini? |
20. | Moabu ameaibishwa, kwa maana amevunjika; Pigeni yowe na kulia; Tangazeni habari hii katika Arnoni, Ya kuwa Moabu ameharibika. |
21. | Na hukumu imeifikilia nchi tambarare; juu ya Holoni, na juu ya Yasa, na juu ya Mefaathi; |
22. | na juu ya Diboni, na juu ya Nebo, na juu ya Beth-diblathaimu; |
23. | na juu ya Kiriathaimu, na juu ya Beth-gamuli, na juu ya Beth-meoni; |
24. | na juu ya Keriothi, na juu ya Bozra, na juu ya miji yote ya nchi ya Moabu, iliyo mbali na iliyo karibu. |
25. | Pembe ya Moabu imekatika, na mkono wake umevunjika, asema Bwana. Mlevyeni; kwa maana alijitukuza juu ya Bwana |
26. | na Moabu atagaa-gaa katika matapiko yake, naye atadhihakiwa. Kwa maana Israeli, je! Hakuwa dhihaka kwako? |
27. | Alionekana kati ya wevi? Maana kila umtajapo watikisa kichwa chako. |
28. | Enyi mkaao Moabu, iacheni miji, Enendeni kukaa majabalini; Mkawe kama njiwa afanyaye kioto chake Katika ubavu wa mdomo wa shimo. |
29. | Tumesikia habari za kiburi cha Moabu; Ya kuwa ana kiburi kingi; Jeuri yake, na kiburi chake, na majivuno yake, Na jinsi alivyotakabari moyoni mwake. |
30. | Najua ghadhabu yake, asema Bwana, ya kuwa si kitu; majisifu yake hayakutenda neno lo lote. |
31. | Kwa sababu hiyo nitampigia yowe Moabu, naam, nitapiga kelele kwa ajili ya Moabu yote; nitawaombolezea watu wa Kir-heresi. |
32. | Nitakulilia, Ee mzabibu wa Sibma, kwa vilio vipitavyo vilio vya Yazeri; matawi yako yalipita juu ya bahari, yalifika hata bahari ya Yazeri; atekaye nyara ameyaangukia matunda yako ya wakati wa jua, na mavuno yako ya zabibu. |
33. | Furaha na shangwe zimeondoshwa, katika shamba lizaalo sana, na katika nchi ya Moabu; nami nimeikomesha divai katika mashinikizo; hapana mtu atakayekanyaga zabibu kwa shangwe; shangwe ile itakuwa si shangwe. |
34. | Toka kilio cha Heshboni mpaka Eleale, naam, mpaka Yahasa, wametoa sauti zao, toka Soari mpaka Horonaimu, hata Eglath-shelishia; maana maji ya Nimrimu nayo yatakuwa ukiwa. |
35. | Pamoja na hayo, asema Bwana, nitamkomesha katika Moabu mtu atoaye sadaka katika mahali pa juu, naye awafukiziaye uvumba miungu yake. |
36. | Kwa sababu hiyo moyo wangu watoa sauti kama filimbi kwa ajili ya Moabu, na kwa ajili ya watu wa Kir-heresi, moyo wangu watoa sauti kama filimbi; kwa kuwa wingi aliojipatia umepotea. |
37. | Maana kila kichwa kina upaa, na ndevu zote zimenyolewa; mikono yote ina alama za chale, na viuno vyote vimevikwa nguo za magunia. |
38. | Juu ya dari zote za nyumba za Moabu, na katika njia kuu zake, pana maombolezo, kila mahali; kwa maana nimevunja Moabu kama chombo kisichopendeza, asema Bwana. |
39. | Jinsi alivyovunjika! Pigeni yowe! Jinsi Moabu alivyogeuza kisogo kwa haya! Hivyo ndivyo Moabu atakavyokuwa dhihaka, na sababu ya kuwashangaza watu wote wamzungukao. |
40. | Maana Bwana asema hivi, Tazama, ataruka kama tai, na kutandaza mabawa yake juu ya Moabu. |
41. | Miji imetwaliwa, ngome zimeshambuliwa, na mioyo ya mashujaa wa Moabu siku hiyo itakuwa kama moyo wa mwanamke katika utungu wake. |
42. | Na Moabu ataangamizwa, asiwe taifa tena, kwa sababu alijitukuza juu ya Bwana. |
43. | Hofu, na shimo, na mtego, zaja juu yako, Ee mwenyeji wa Moabu, asema Bwana. |
44. | Aikimbiaye hofu ataanguka shimoni; na yeye atokaye shimoni atanaswa kwa mtego; maana nitaleta juu yake, yaani, juu ya Moabu, mwaka wa kujiliwa kwake, asema Bwana. |
45. | Wamekimbia, wasio na nguvu Wanasimama chini ya kivuli cha Heshboni; Ila moto umetoka katika Heshboni, Na mwali wa moto toka kati ya Sihoni Nao umekula pembe ya Moabu, Na utosi wa kichwa wa watu wapigao kelele. |
46. | Ole wako! Ee Moabu, Watu wa Kemoshi wamepotea; Maana wana wako wamechukuliwa mateka, Na binti zako wamekwenda utumwani. |
47. | Lakini nitawarudisha watu wa Moabu walio utumwani, siku za mwisho, asema Bwana. Hukumu ya Moabu imefikilia hapa. |
← Jeremiah (48/52) → |