Jeremiah (44/52)  

1. Neno lililomjia Yeremia, katika habari za Wayahudi wote waliokaa katika nchi ya Misri, waliokaa Migdoli, na Tahpanesi, na Nofu, na katika nchi ya Pathrosi, kusema,
2. Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Ninyi mmeona mabaya yote niliyoleta juu ya Yerusalemu, na juu ya miji yote ya Yuda; na, tazama, ni ukiwa leo, wala hapana mtu akaaye ndani yake;
3. kwa sababu ya uovu wao, waliotenda ili kunikasirisha, kwa kuwa walikwenda kufukiza uvumba, na kuwatumikia miungu mingine, ambao hawakuwajua, wao, wala ninyi, wala baba zenu.
4. Tena nalituma kwenu watumishi wangu wote, manabii, nikiamka mapema na kuwatuma, nikisema, Basi ninyi; msilifanye chukizo hili linichukizalo.
5. Lakini hawakusikiliza, wala hawakutega masikio yao, ili wageuke na kuacha uovu wao, wasifukizie uvumba miungu mingine.
6. Kwa sababu hiyo ghadhabu yangu, na hasira yangu, zilimwagika, nazo ziliwaka katika miji ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu, na miji hiyo imeachwa ukiwa, na kuharibika, kama ilivyo leo.
7. Basi, sasa, Bwana, Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Kwa nini mnafanya uovu huu mkubwa juu ya nafsi zenu wenyewe, kujikatilia mbali mwanamume na mwanamke, mtoto mchanga na anyonyaye, mtoke kati ya Yuda, msijiachie mtu abakiye;
8. kwa kuwa mnanikasirisha kwa matendo ya mikono yenu, mkifukizia uvumba miungu mingine katika nchi ya Misri, mlikokwenda kukaa ugenini; mpate kukatiliwa mbali, na kuwa laana, na aibu, katika mataifa yote ya dunia?
9. Je! Mmeusahau uovu wa baba zenu, na uovu wa wafalme wa Yuda, na uovu wa wake zao, na uovu wenu wenyewe, na uovu wa wake zenu, walioutenda katika nchi ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu?
10. Hawajanyenyekea hata leo, wala hawakuogopa, wala hawakuenenda katika sheria yangu, wala katika amri zangu, nilizoweka mbele yenu, na mbele ya baba zenu.
11. Basi, kwa sababu hiyo Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Tazama, nitaelekeza uso wangu juu yenu, ili niwaletee mabaya, hata kukatilia mbali Yuda yote.
12. Nami nitawatwaa mabaki ya Yuda, walioelekeza nyuso zao kuiingia nchi ya Misri, wakae huko, nao wataangamia wote pia; wataanguka katika nchi ya Misri; wataangamia kwa upanga, na kwa njaa; watakufa, tangu wadogo hata wakubwa, kwa upanga, na kwa njaa; nao watakuwa apizo, na ajabu, na laana, na aibu.
13. Kwa maana nitawaadhibu wakaao katika nchi ya Misri, kama nilivyouadhibu Yerusalemu, kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni;
14. hata katika watu wale wa Yuda waliosalia, waliokwenda nchi ya Misri ili wakae huko, hapatakuwa na mtu ye yote atakayepona, wala atakayesalia, na kupata kurudi nchi ya Yuda, ambayo wanatamani kurudi ili kukaa huko; maana hapana atakayerudi, ila wao watakaopona.
15. Ndipo watu wote waliojua ya kuwa wake zao waliwafukizia uvumba miungu mingine, na wanawake wote waliosimama karibu, mkutano mkubwa, yaani, watu wote waliokaa katika nchi ya Misri, katika Pathrosi, wakamjibu Yeremia, wakisema,
16. Neno lile ulilotuambia kwa jina la Bwana, sisi hatutakusikiliza.
17. Lakini bila shaka tutalitimiza kila neno lililotoka katika vinywa vyetu, kumfukizia uvumba malkia wa mbinguni, na kummiminia sadaka za kinywaji, kama tulivyotenda sisi, na baba zetu, na wafalme wetu, na wakuu wetu, katika miji ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu; maana wakati huo tulikuwa na chakula tele, na kufanikiwa, wala hatukuona mabaya.
18. Lakini tulipoacha kumfukizia uvumba malkia wa mbinguni, na kummiminia sadaka za kinywaji, tumepungukiwa na vitu vyote; na kuangamizwa kwa upanga, na kwa njaa.
19. Nasi tulipomfukizia uvumba malkia wa mbinguni, na kummiminia sadaka za kinywaji, je! Tulimfanyizia mikate, ili kumwabudu, na kummiminia mamiminiko, waume zetu wasipokuwapo?
20. Ndipo Yeremia akawaambia watu wote, wanaume na wanawake, yaani, watu wote waliompa jibu lile, akisema,
21. Uvumba mliofukiza katika miji ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu, ninyi, na baba zenu, wafalme wenu, na wakuu wenu, na watu wa nchi, je! Bwana hakuwakumbuka watu hao? Je! Jambo hili halikuingia moyoni mwake?
22. Hata Bwana asiweze kuvumilia tena, kwa sababu ya uovu wa matendo yenu, na kwa sababu ya machukizo mliyoyafanya; kwa sababu hiyo nchi yenu imekuwa ukiwa, na ajabu, na laana, isikaliwe na mtu kama ilivyo leo.
23. Kwa sababu mmefukiza uvumba, na kwa sababu mmetenda dhambi juu ya Bwana, wala hamkuitii sauti ya Bwana, wala hamkwenda katika torati yake, wala katika amri zake, wala katika shuhuda yake; ndiyo maana mabaya haya yamewapata kama ilivyo leo.
24. Tena Yeremia akawaambia watu wote, na wanawake wote, Lisikieni neno hili la Bwana, ninyi nyote wa Yuda, mliopo hapa katika nchi ya Misri;
25. Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Ninyi na wake zenu mmenena kwa vinywa vyenu, na kutimiza kwa mikono yenu, mkisema, Bila shaka tutazitimiza nadhiri zetu tulizoziweka, na kumfukizia uvumba malkia wa mbinguni, na kummiminia sadaka za kinywaji; basi, zithibitisheni nadhiri zenu, zitimizeni nadhiri zenu.
26. Basi, kwa sababu hiyo lisikieni neno la Bwana, ninyi nyote wa Yuda, mnaokaa katika nchi ya Misri, Tazama, nimeapa kwa jina langu kuu, asema Bwana, ya kwamba jina langu halitatajwa tena katika kinywa cha mtu awaye yote wa Yuda, katika nchi yote ya Misri, akisema, Kama Bwana MUNGU aishivyo!
27. Tazama, nawaangalia niwaletee mabaya, wala si mema; nao watu wote wa Yuda, waliopo hapa katika nchi ya Misri, wataangamizwa kwa upanga, na kwa njaa, hata wakomeshwe kabisa.
28. Nao watakaoukimbia upanga, watatoka katika nchi ya Misri, na kuiingia nchi ya Yuda, watu wachache sana; na wote wa Yuda waliosalia, waliokwenda nchi ya Misri ili kukaa huko, watajua ni neno la nani litakalosimama, neno langu, au neno lao.
29. Na hii ndiyo itakayokuwa ishara kwenu, asema Bwana, kwamba mimi nitawaadhibu ninyi mahali hapa, mpate kujua ya kuwa maneno yangu yatasimama juu yenu, kuwaletea mabaya bila shaka;
30. Bwana asema hivi, Tazama, nitamtia Farao Hofra, mfalme wa Misri, katika mikono ya adui zake, na katika mikono yao wamtafutao roho yake; kama vile nilivyomtia Sedekia, mfalme wa Yuda, katika mikono ya Nebukadreza, mfalme wa Babeli, adui yake aliyemtafuta roho yake.

  Jeremiah (44/52)