← Jeremiah (42/52) → |
1. | Ndipo maakida wote wa majeshi, na Yohana, mwana wa Karea, na Yezania, mwana wa Hoshaya, na watu wote tangu wadogo hata wakubwa, wakakaribia, |
2. | wakamwambia Yeremia, nabii, Twakusihi, maombi yetu yakubaliwe mbele yako, ukatuombee kwa Bwana, Mungu wako, yaani, watu hawa wote waliosalia; maana tumesalia wachache tu katika watu wengi, kama macho yako yatuonavyo; |
3. | ili kwamba Bwana, Mungu wako, atuonyeshe njia ambayo yatupasa tuiendee, na jambo litupasalo tulitende. |
4. | Ndipo Yeremia, nabii, akawaambia, Nimewasikia; tazama, nitamwomba Bwana, Mungu wenu, sawasawa na maneno yenu; tena itakuwa, neno lo lote ambalo Bwana atawajibu, nitawaambia; sitawazuilia neno liwalo lote. |
5. | Wakamwambia Yeremia, Bwana na awe shahidi wa kweli na uaminifu kati yetu; ikiwa hatufanyi sawasawa na neno lile, ambalo Bwana, Mungu wako, atakutuma utuletee. |
6. | Likiwa jema, au likiwa baya, sisi tutaitii sauti ya Bwana, Mungu wetu, ambaye tunakutuma kwake; ipate kuwa faida yetu, tunapoitii sauti ya Bwana, Mungu wetu. |
7. | Ikawa, baada ya siku kumi, neno la Bwana likamjia Yeremia. |
8. | Ndipo akamwita Yohana, mwana wa Karea, na maakida wote wa majeshi waliokuwa pamoja naye, na watu wote tangu wadogo hata wakubwa, |
9. | akawaambia, Bwana, Mungu wa Israeli, ambaye mlinituma kwake, ili niyaweke maombi yenu mbele yake, asema hivi; |
10. | Ikiwa mtakaa bado katika nchi hii, ndipo nitawajenga, wala sitawabomoa, nami nitawapanda, wala sitawang'oa; kwa maana nayajutia mabaya niliyowatenda. |
11. | Msimwogope mfalme wa Babeli, mnayemwogopa; msimwogope, asema Bwana; maana mimi ni pamoja nanyi, niwaokoe, na kuwaponya na mkono wake. |
12. | Nami nitawapa rehema, kwamba awarehemu ninyi, na kuwarudisha mkae katika nchi yenu wenyewe. |
13. | Lakini mkisema, Hatutaki kukaa katika nchi hii; msiitii sauti ya Bwana, Mungu wenu; |
14. | mkisema, La! Lakini tutakwenda nchi ya Misri, ambayo hatutaona vita, wala kuisikia sauti ya tarumbeta, wala kuona njaa kwa kukosa chakula; nasi tutakaa huko; |
15. | basi, lisikieni neno la Bwana, enyi mabaki ya Yuda; Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Ikiwa mwakaza nyuso zenu kuingia Misri, na kwenda kukaa huko; |
16. | basi, itakuwa, upanga mnaouogopa utawapata huko, katika nchi ya Misri, nayo njaa mnayoiogopa itawafuatia mbio huko Misri, nanyi mtakufa huko. |
17. | Haya ndiyo yatakayowapata watu wote waelekezao nyuso zao kwenda Misri, na kukaa huko; watakufa kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni; hapana mtu awaye yote miongoni mwao atakayesalia, au kuokoka katika mabaya nitakayoyaleta juu yao. |
18. | Maana Bwana wa majeshi Mungu wa Israeli, asema hivi, Kama hasira yangu, na ghadhabu yangu, ilivyomwagwa juu ya hao wakaao Yerusalemu, ndivyo ghadhabu yangu itakavyomwagwa juu yenu, mtakapoingia Misri; nanyi mtakuwa apizo, na ajabu, na laana, na aibu; wala hamtapaona mahali hapa tena. |
19. | Bwana asema katika habari zenu, enyi mabaki ya Yuda, Msiingie Misri; jueni sana ya kuwa nimewashuhudia hivi leo. |
20. | Maana mmetenda kwa hila juu ya nafsi zenu wenyewe; kwa kuwa mmenituma kwa Bwana, Mungu wenu, mkisema, Utuombee kwa Bwana, Mungu wetu, ukatufunulie sawasawa na yote atakayoyanena Bwana, Mungu wetu, nasi tutayatenda; |
21. | nami nimewafunulia haya leo; lakini ninyi hamkuitii sauti ya Bwana, Mungu wenu, katika neno lo lote ambalo amenituma kwenu. |
22. | Basi, sasa jueni sana ya kuwa mtakufa kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni, katika mahali pale mnapopatamani kwenda na kukaa. |
← Jeremiah (42/52) → |