Jeremiah (27/52)  

1. Mwanzo wa kumiliki kwake Sedekia, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, neno hili likamjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, kusema,
2. Bwana ameniambia hivi, Jifanyizie vifungo na nira, ukajivike shingoni;
3. kisha uvipeleke kwa mfalme wa Edomu, na mfalme wa Moabu, na mfalme wa wana wa Amoni, na mfalme wa Tiro, na mfalme wa Sidoni, kwa mikono ya wajumbe watakaofika Yerusalemu kwa Sedekia, mfalme wa Yuda.
4. Uwaagize waende kwa bwana zao, na kuwaambia, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Mtawaambia bwana zenu maneno haya;
5. Mimi nimeiumba dunia hii, wanadamu na wanyama walio juu ya uso wa nchi, kwa uweza wangu mkuu, na kwa mkono wangu ulionyoshwa; nami nawapa watu kama inipendezavyo.
6. Na sasa nimetia nchi hizi zote katika mkono wa Nebukadreza, mfalme wa Babeli, mtumishi wangu; na wanyama wa mwituni pia nimempa wamtumikie.
7. Na mataifa yote watamtumikia yeye, na mwanawe, na mwana wa mwanawe, hata utakapowadia wakati wa nchi yake mwenyewe, ndipo mataifa mengi na wafalme wakuu watamtumikisha yeye.
8. Na itakuwa, taifa lile na mfalme yule asiyetaka kumtumikia Nebukadreza, huyo mfalme wa Babeli, na kutia shingo zao katika nira ya mfalme wa Babeli, mimi nitaliadhibu taifa lile kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni, asema Bwana, hata nitakapokuwa nimewaangamiza kwa mkono wake.
9. Lakini, katika habari zenu, msisikilize manabii wenu, wala wabashiri wenu, wala ndoto zenu, wala watambuzi wenu, wala waganga wenu, wanaowaambia, ya kwamba, Hamtamtumikia mfalme wa Babeli;
10. maana wanawatabiria uongo, ili kuwatoa ninyi mbali na nchi yenu; niwafukuze mkaangamie.
11. Bali taifa lile watakaotia shingo zao katika nira ya mfalme wa Babeli, na kumtumikia, taifa hilo nitawaacha wakae katika nchi yao wenyewe, asema Bwana; nao watailima, na kukaa ndani yake.
12. Nikamwambia Sedekia, mfalme wa Yuda, kwa mfano wa maneno hayo yote, nikisema, Tieni shingo zenu katika nira ya mfalme wa Babeli, mkamtumikie yeye na watu wake, mpate kuishi.
13. Mbona mnataka kufa, wewe na watu wako, kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni, kama Bwana alivyosema katika habari ya taifa lile, lisilotaka kumtumikia mfalme wa Babeli?
14. Wala msisikilize maneno ya manabii wawaambiao ninyi, ya kwamba, Hamtamtumikia mfalme wa Babeli; maana wanawatabiria uongo.
15. Kwa maana mimi sikuwatuma, asema Bwana, bali wanatabiri uongo kwa jina langu; nipate kuwatoeni nje, mkaangamie, ninyi, na manabii hao wanaowatabiria.
16. Pia nalisema na makuhani, na watu wote, nikisema, Bwana asema hivi, Msisikilize maneno ya manabii wenu, wanaowatabiria, wakisema, Tazameni, vyombo vya nyumba ya Bwana, baada ya muda kidogo, vitaletwa tena toka Babeli; maana wanawatabiria uongo.
17. Msiwasikilize; mtumikieni mfalme wa Babeli, mkaishi; kwani mji huu kufanywa ukiwa?
18. Lakini ikiwa hao ni manabii, na ikiwa neno la Bwana liko kwao, basi na wamwombe Bwana wa majeshi, kwamba vyombo vile vilivyosalia katika nyumba ya Bwana, na katika nyumba ya mfalme wa Yuda, na hapa Yerusalemu, visiende Babeli.
19. Maana Bwana wa majeshi asema hivi, katika habari za nguzo, na katika habari za bahari, na katika habari za matako yake, na katika habari za mabaki ya vyombo vilivyoachwa katika mji huu,
20. ambavyo Nebukadreza, mfalme wa Babeli, hakuvichukua, hapo alipomchukua Yekonia, mwana wa Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, toka Yerusalemu mpaka Babeli, pamoja na wakuu wote wa Yuda, na Yerusalemu;
21. naam, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, katika habari za vyombo vilivyobaki katika nyumba ya Bwana, na katika nyumba ya mfalme wa Yuda, na hapa Yerusalemu;
22. Vitachukuliwa mpaka Babeli, navyo vitakaa huko, hata siku ile nitakapovijilia, asema Bwana; hapo ndipo nitakapovileta tena, na kuvirudisha mahali hapa.

  Jeremiah (27/52)