| ← Hebrews (10/13) → |
| 1. | Basi torati, kwa kuwa ni kivuli cha mema yatakayokuwa, wala si sura yenyewe ya mambo hayo, kwa dhabihu zile zile wanazozitoa kila mwaka daima, haiwezi wakati wo wote kuwakamilisha wakaribiao. |
| 2. | Kama ndivyo, je! Dhabihu hazingekoma kutolewa; kwa maana waabuduo, wakiisha kusafishwa mara moja, wasingejiona tena kuwa na dhambi? |
| 3. | Lakini katika dhabihu hizo liko kumbukumbu la dhambi kila mwaka. |
| 4. | Maana haiwezekani damu ya mafahali na mbuzi kuondoa dhambi. |
| 5. | Kwa hiyo ajapo ulimwenguni, asema, Dhabihu na toleo hukutaka, Lakini mwili uliniwekea tayari; |
| 6. | Sadaka za kuteketezwa na sadaka za dhambi hukupendezwa nazo; |
| 7. | Ndipo niliposema, Tazama, nimekuja (katika gombo la chuo nimeandikiwa) Niyafanye mapenzi yako, Mungu. |
| 8. | Hapo juu asemapo, Dhabihu na matoleo na sadaka za kuteketezwa na hizo za dhambi hukuzitaka, wala hukupendezwa nazo (zitolewazo kama ilivyoamuru torati), |
| 9. | ndipo aliposema, Tazama, nimekuja niyafanye mapenzi yako. Aondoa la kwanza, ili kusudi alisimamishe la pili. |
| 10. | Katika mapenzi hayo mmepata utakaso, kwa kutolewa mwili wa Yesu Kristo mara moja tu. |
| 11. | Na kila kuhani husimama kila siku akifanya ibada, na kutoa dhabihu zile zile mara nyingi; ambazo haziwezi kabisa kuondoa dhambi. |
| 12. | Lakini huyu, alipokwisha kutoa kwa ajili ya dhambi dhabihu moja idumuyo hata milele, aliketi mkono wa kuume wa Mungu; |
| 13. | tangu hapo akingojea hata adui zake wawekwe kuwa chini ya miguu yake. |
| 14. | Maana kwa toleo moja amewakamilisha hata milele hao wanaotakaswa. |
| 15. | Na Roho Mtakatifu naye amshuhudia; kwa maana, baada ya kusema, |
| 16. | Hili ni agano nitakaloagana nao baada ya siku zile, anena Bwana, Nitatia sheria zangu mioyoni mwao, Na katika nia zao nitaziandika; |
| 17. | Dhambi zao na uasi wao sitaukumbuka tena kabisa. |
| 18. | Basi, ondoleo la hayo likiwapo, hapana toleo tena kwa ajili ya dhambi. |
| 19. | Basi, ndugu, kwa kuwa tuna ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu, |
| 20. | njia ile aliyotuanzia iliyo mpya, iliyo hai, ipitayo katika pazia, yaani, mwili wake; |
| 21. | na kuwa na kuhani mkuu juu ya nyumba ya Mungu; |
| 22. | na tukaribie wenye moyo wa kweli, kwa utimilifu wa imani, hali tumenyunyiziwa mioyo tuache dhamiri mbaya, tumeoshwa miili kwa maji safi. |
| 23. | Na mlishike sana ungamo la tumaini letu, lisigeuke; maana yeye aliyeahidi ni mwaminifu; |
| 24. | tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; |
| 25. | wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia. |
| 26. | Maana, kama tukifanya dhambi kusudi baada ya kuupokea ujuzi wa ile kweli, haibaki tena dhabihu kwa ajili ya dhambi; |
| 27. | bali kuna kuitazamia hukumu yenye kutisha, na ukali wa moto ulio tayari kuwala wao wapingao. |
| 28. | Mtu aliyeidharau sheria ya Musa hufa pasipo huruma, kwa neno la mashahidi wawili au watatu. |
| 29. | Mwaonaje? Haikumpasa adhabu iliyo kubwa zaidi mtu yule aliyemkanyaga Mwana wa Mungu, na kuihesabu damu ya agano aliyotakaswa kwayo kuwa ni kitu ovyo, na kumfanyia jeuri Roho wa neema? |
| 30. | Maana twamjua yeye aliyesema, Kupatiliza kisasi ni juu yangu, mimi nitalipa. Na tena, Bwana atawahukumu watu wake. |
| 31. | Ni jambo la kutisha kuanguka katika mikono ya Mungu aliye hai. |
| 32. | Lakini zikumbukeni siku za kwanza, ambazo, mlipokwisha kutiwa nuru, mlistahimili mashindano makubwa ya maumivu; |
| 33. | pindi mlipotwezwa kwa mashutumu na dhiki, na pindi mliposhirikiana na wale waliotendewa hayo. |
| 34. | Maana mliwaonea huruma wale waliokuwa katika vifungo, tena mkakubali kwa furaha kunyang'anywa mali zenu, mkijua kwamba nafsini mwenu mna mali iliyo njema zaidi, idumuyo. |
| 35. | Basi msiutupe ujasiri wenu, kwa maana una thawabu kuu. |
| 36. | Maana mnahitaji saburi, ili kwamba mkiisha kuyafanya mapenzi ya Mungu mpate ile ahadi. |
| 37. | Kwa kuwa bado kitambo kidogo sana, Yeye ajaye atakuja, wala hatakawia. |
| 38. | Lakini mwenye haki wangu ataishi kwa imani; Naye akisita-sita, roho yangu haina furaha naye. |
| 39. | Lakini sisi hatumo miongoni mwao wasitao na kupotea, bali tumo miongoni mwa hao walio na imani ya kutuokoa roho zetu. |
| ← Hebrews (10/13) → |