Galatians (5/6)  

1. Katika ungwana huo Kristo alituandika huru; kwa hiyo simameni, wala msinaswe tena chini ya kongwa la utumwa.
2. Tazama, mimi Paulo nawaambia ninyi ya kwamba, mkitahiriwa, Kristo hatawafaidia neno.
3. Tena namshuhudia kila mtu atahiriwaye, kwamba ni wajibu wake kuitimiza torati yote.
4. Mmetengwa na Kristo, ninyi mtakao kuhesabiwa haki kwa sheria; mmeanguka na kutoka katika hali ya neema.
5. Maana sisi kwa Roho tunalitazamia tumaini la haki kwa njia ya imani.
6. Maana katika Kristo Yesu kutahiriwa hakufai neno, wala kutokutahiriwa, bali imani itendayo kazi kwa upendo.
7. Mlikuwa mkipiga mbio vizuri; ni nani aliyewazuia msiitii kweli?
8. Kushawishi huku hakukutoka kwake yeye anayewaita ninyi.
9. Chachu kidogo huchachua donge zima.
10. Nina matumaini kwenu katika Bwana, ya kwamba hamtakuwa na nia ya namna nyingine. Lakini yeye anayewafadhaisha atachukua hukumu yake, awaye yote.
11. Nami, ndugu zangu ikiwa ninahubiri habari ya kutahiriwa, kwa nini ningali ninaudhiwa? Hapo kwazo la msalaba limebatilika!
12. Laiti hao wanaowatia mashaka wangejikata nafsi zao!
13. Maana ninyi, ndugu, mliitwa mpate uhuru; lakini uhuru wenu usiwe sababu ya kuufuata mwili, bali tumikianeni kwa upendo.
14. Maana torati yote imetimilika katika neno moja, nalo ni hili, Umpende jirani yako kama nafsi yako.
15. Lakini mkiumana na kulana, angalieni msije mkaangamizana.
16. Basi nasema, Enendeni kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili.
17. Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka.
18. Lakini mkiongozwa na Roho, hampo chini ya sheria.
19. Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi,
20. ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi,
21. husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.
22. Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu,
23. upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.
24. Na hao walio wa Kristo Yesu wameusulibisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake.
25. Tukiishi kwa Roho, na tuenende kwa Roho.
26. Tusijisifu bure, tukichokozana na kuhusudiana.

  Galatians (5/6)