Exodus (27/40)  

1. Nawe fanya madhabahu ya mti wa mshita; urefu wake utakuwa ni dhiraa tano, na upana wake dhiraa tano; hiyo madhabahu itakuwa mraba; na kwenda juu kwake kutakuwa dhiraa tatu.
2. Nawe fanya pembe nne katika pembe zake nne; hizo pembe zitakuwa za kitu kimoja na madhabahu; nawe utayafunika shaba.
3. Na vyombo vyake vya kuyaondoa majivu yake utavifanya, na majembe yake, na mabakuli yake, na uma zake, na meko yake; vyombo vyake vyote utavifanya vya shaba.
4. Nawe uifanyie hiyo madhabahu wavu wa shaba; kisha utie pete nne za shaba katika hizo pembe nne za ule wavu.
5. Nawe tia huo wavu chini ya kizingo kiizungukacho madhabahu upande wa chini, ili huo wavu ufikilie katikati ya hiyo madhabahu.
6. Nawe fanya miti kwa ajili ya madhabahu, miti ya mshita, na kuifunika shaba.
7. Na hiyo miti itatiwa katika pete, na ile miti itakuwa katika pande mbili za madhabahu, wakati wa kuichukua.
8. Uifanye ya mbao, yenye mvungu ndani yake; kama ulivyoonyeshwa mlimani, ndivyo watakavyoifanya.
9. Nawe fanya ua wa maskani; upande wa kusini wa kuelekea kusini kutakuwa na chandarua ya nguo ya kitani nzuri yenye kusokotwa, kwa huo ua, urefu wake upande mmoja utakuwa ni dhiraa mia;
10. na nguzo zake zitakuwa nguzo ishirini, na matako yake ishirini, matako yake yatakuwa ya shaba; kulabu za zile nguzo na vitanzi vyake vitakuwa vya fedha.
11. Ni vivyo upande wa kaskazini, urefu wake hiyo chandarua utakuwa ni dhiraa mia, na nguzo zake ishirini, na matako yake ishirini yatakuwa ya shaba; kulabu za zile nguzo na vitanzi vyake vitakuwa vya fedha.
12. Na upande wa magharibi, upana wa ua kutakuwa na chandarua ya dhiraa hamsini; nguzo zake kumi, na matako yake kumi.
13. Na upana wa ule ua upande wa mashariki kuelekea mashariki utakuwa ni dhiraa hamsini.
14. Chandarua upande mmoja wa lango itakuwa dhiraa kumi na tano upana wake; nguzo zake zitakuwa tatu na matako yake matatu.
15. Upande wa pili ni vivyo chandarua ya dhiraa kumi na tano; nguzo zake tatu, na matako yake matatu.
16. Na kwa lile lango la ua patakuwa na kisitiri cha dhiraa ishirini, kitakuwa cha nguo ya rangi ya samawi, na ya rangi ya zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri yenye kusokotwa, kazi ya mshona taraza; nguzo zake zitakuwa nne, na matako yake manne.
17. Nguzo zote za ule ua ziuzungukazo pande zote zitakuwa na vitanzi vya fedha; kulabu zake za fedha, na matako yake ya shaba.
18. Urefu wa huo ua utakuwa dhiraa mia, na upana wake utakuwa dhiraa hamsini kotekote, na kwenda juu kwake dhiraa tano; yawe ya nguo ya kitani nzuri, na matako yake yatakuwa ya shaba.
19. Vyombo vyote vya maskani vitumiwavyo katika utumishi wake wote, na vigingi vyake vyote, na vigingi vyote vya ule ua, vitakuwa vya shaba.
20. Nawe waamuru wana wa Israeli wakuletee mafuta ya zeituni safi ya kupondwa kwa ajili ya nuru, ili kufanya ile taa kuwaka daima.
21. Ndani ya ile hema ya kukutania, nje ya hilo pazia, lililo mbele ya huo ushuhuda, Haruni na wanawe wataitengeza tangu jioni hata asubuhi mbele ya Bwana; itakuwa ni amri ya milele katika vizazi vyao vyote kwa ajili ya wana wa Israeli.

  Exodus (27/40)