Ephesians (5/6)  

1. Hivyo mfuateni Mungu, kama watoto wanaopendwa;
2. mkaenende katika upendo, kama Kristo naye alivyowapenda ninyi tena akajitoa kwa ajili yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu, kuwa harufu ya manukato.
3. Lakini uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wa kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu;
4. wala aibu wala maneno ya upuzi wala ubishi; hayo hayapendezi; bali afadhali kushukuru.
5. Maana neno hili mnalijua hakika, ya kwamba hakuna mwasherati wala mchafu wala mwenye tamaa, ndiye mwabudu sanamu, aliye na urithi katika ufalme wa Kristo na Mungu.
6. Mtu asiwadanganye kwa maneno yasiyo na maana; kwa kuwa kwa sababu ya hayo hasira ya Mungu huwajia wana wa uasi.
7. Basi msishirikiane nao.
8. Kwa maana zamani ninyi mlikuwa giza, bali sasa mmekuwa nuru katika Bwana; enendeni kama watoto wa nuru,
9. kwa kuwa tunda la nuru ni katika wema wote na haki na kweli;
10. mkihakiki ni nini impendezayo Bwana.
11. Wala msishirikiane na matendo yasiyozaa ya giza, bali myakemee;
12. kwa kuwa yanayotendeka kwao kwa siri, ni aibu hata kuyanena.
13. Lakini yote yaliyokemewa hudhihirishwa na nuru maana kila kilichodhihirika ni nuru.
14. Hivyo husema, Amka, wewe usinziaye, Ufufuke katika wafu, Na Kristo atakuangaza.
15. Basi angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima;
16. mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu.
17. Kwa sababu hiyo msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyo mapenzi ya Bwana.
18. Tena msilewe kwa mvinyo, ambamo mna ufisadi; bali mjazwe Roho;
19. mkisemezana kwa zaburi na tenzi na nyimbo za rohoni, huku mkiimba na kumshangilia Bwana mioyoni mwenu;
20. na kumshukuru Mungu Baba sikuzote kwa mambo yote, katika jina lake Bwana wetu Yesu Kristo;
21. hali mnanyenyekeana katika kicho cha Kristo.
22. Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu.
23. Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili.
24. Lakini kama vile Kanisa limtiivyo Kristo vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo.
25. Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake;
26. ili makusudi alitakase na kulisafisha kwa maji katika neno;
27. apate kujiletea Kanisa tukufu, lisilo na ila wala kunyanzi wala lo lote kama hayo; bali liwe takatifu lisilo na mawaa.
28. Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe.
29. Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, kama Kristo naye anavyolitendea Kanisa.
30. Kwa kuwa tu viungo vya mwili wake.
31. Kwa sababu hiyo mtu atamwacha baba yake na mama yake, ataambatana na mkewe na hao wawili watakuwa mwili mmoja.
32. Siri hiyo ni kubwa; ila mimi nanena habari ya Kristo na Kanisa.
33. Lakini kila mtu ampende mke wake kama nafsi yake mwenyewe; wala mke asikose kumstahi mumewe.

  Ephesians (5/6)