Deuteronomy (21/34)  

1. Aonekanapo mtu ameuawa katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako, kuimiliki, amelala kondeni, wala haijulikani ni nani aliyempiga;
2. na watoke nje wazee wako na waamuzi wako, nao wapime hapo mpaka miji iliyomzunguka huyo aliyeuawa;
3. na iwe, mji ulio karibu na yule aliyeuawa, wale wazee wake mji huo watwae mtamba katika kundi la ng'ombe, ambaye hajafanya kazi, wala hajakokota jembe la nira;
4. wazee wa mji huo na wamshushe yule mtamba mpaka bonde lenye maji ya mtoni, lisilolimwa wala kupandwa, wakamvunje yule mtamba shingo yake humo bondeni;
5. nao makuhani wana wa Lawi wasongee karibu, kwa kuwa ndio aliowachagua Bwana, Mungu wako, wamtumikie, na kubariki katika jina la Bwana na kila neno lishindaniwalo, na kila pigo, litakuwa kwa kufuata maneno yao;
6. na wazee wote wa mji ule, ulio karibu sana na yule aliyeuawa, na waoshe mikono yao juu ya huyo mtamba aliyevunjwa shingo yake humo bondeni;
7. na wajibizane kwamba, Mikono yetu haikumwaga damu hii, wala macho yetu hayakuiona.
8. Ee Bwana, samehe watu wako Israeli, uliowakomboa, wala usiache damu ya asiye makosa ikakaa katikati ya watu wako Israeli. Na ile damu utasamehewa kwao.
9. Ndivyo utakavyoondoa damu ya asiye makosa katikati yako, utakapofanya yaliyo sawa machoni pa Bwana.
10. Utakapokwenda vitani kupigana juu ya adui zako, na Bwana, Mungu wako, awatiapo mikononi mwako, nawe uwachukuapo mateka,
11. ukaona kati ya mateka mwanamke mzuri, ukafanya tamaa kwake, ukawaza kumtwaa kuwa mkeo;
12. ndipo umchukue kwenu nyumbani kwako, naye atanyoa kichwa, akate na kucha;
13. avue na mavazi ya uteka wake akae nyumbani mwako, awakalie matanga babaye na mamaye mwezi mzima, kisha uingie kwake uwe mumewe, naye awe mkeo.
14. Tena utakapokuwa huna furaha naye, mpe ruhusa aende atakako; lakini usimwuze kabisa kwa fedha, usimfanye kama mtumwa, kwa kuwa ulimtweza.
15. Akiwa mtu yuna wake wawili, mmoja ampenda, mmoja hampendi, nao wamemzalia watoto, ampendaye na asiyempenda wote wawili; na yule mzaliwa wa kwanza akiwa ni wa mke asiyependwa;
16. ndipo itakapokuwa ya kwamba siku atakayowarithisha wanawe alivyo navyo, asimweke mwana wa ampendaye kuwa mzaliwa wa kwanza mbele ya mwana wa asiyempenda, naye ndiye mzaliwa wa kwanza huyu;
17. lakini amkubali mzaliwa wa kwanza mwana wa yule asiyempenda, kwa kumpa mafungu mawili katika vyote alivyo navyo; kwa maana ndiye mwanzo wa nguvu zake; haki ya mzaliwa wa kwanza ni yake yeye.
18. Mtu akiwa na mwana mkaidi, mshupavu, asiyetii sauti ya baba yake, wala sauti ya mama yake, nao wajapomwadhibu hawasikizi,
19. ndipo babaye na mamaye na wamkamate, na kumpeleka kwa wazee wa mji wake, katika lango la mahali pake;
20. wawaambie wazee wa mji wake, Huyu mwana wetu ni mkaidi, mshupavu, hasikizi sauti yetu; ni mwasherati, tena ni mlevi.
21. Waume wote wa mji wake na wamtupie mawe, afe; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati yako; na Israeli wote watasikia na kuogopa.
22. Akiwa mtu ametenda dhambi ipasayo kufa, akauawa, nawe ukamtundika juu ya mti;
23. mzoga wake usikae usiku kucha juu ya mti; lazima utamzika siku iyo hiyo; kwani aliyetundikwa amelaaniwa na Mungu; usije ukatia unajisi katika nchi yako akupayo Bwana, Mungu wako, iwe urithi wako.

  Deuteronomy (21/34)