← Deuteronomy (11/34) → |
1. | Kwa ajili hii mpende Bwana, Mungu wako, na kushika sikuzote mausia yake, na amri zake, na hukumu zake, na maagizo yake. |
2. | Nanyi leo jueni; kwa kuwa sisemi sasa na vijana vyenu, ambao hawakujua, wala hawakuona adhabu ya Bwana, Mungu wenu, ukuu wake, na mkono wake wa nguvu, na mkono wake ulionyoka, |
3. | na ishara zake, na kazi zake alizomfanya Farao mfalme wa Misri, na nchi yake yote, katikati ya Misri; |
4. | na alivyolifanya jeshi la Misri, farasi zao, na magari yao; na alivyowafunikiza maji ya Bahari ya Shamu walipokuwa wakiwaandamia, na alivyowaangamiza Bwana hata hivi leo; |
5. | na mambo aliyowafanyia ninyi barani, hata mkaja mahali hapa; |
6. | na alivyowafanya Dathani, na Abiramu, wana wa Eliabu mwana wa Reubeni; nchi ilivyofunua kinywa chake, ikawameza, na walio nyumbani mwao, na mahema yao, na kila kitu kilichokuwa hai kikiwafuata, katikati ya Israeli yote; |
7. | lakini macho yenu yameiona kazi kubwa ya Bwana aliyoifanya, yote. |
8. | Kwa hiyo yaangalieni maagizo yote niwaagizayo leo, mpate kuwa na nguvu, na kuingia mkaimiliki nchi mwivukiayo kuimiliki; |
9. | nanyi mpate kuzifanya siku zenu kuwa nyingi juu ya nchi Bwana aliyowaapia baba zenu, ya kuwa atawapa wao na kizazi chao, nchi imiminikayo maziwa na asali |
10. | Kwa kuwa nchi mwingiayo kuimiliki, si mfano wa nchi ya Misri mlikotoka, uliyokuwa ukipanda mbegu zako humo na kuinywesheleza kwa mguu wako, kama shamba la mboga; |
11. | lakini nchi mwivukiayo kuimiliki ni nchi ya vilima na mabonde, nayo hunyweshwa maji ya mvua ya mbinguni; |
12. | nayo ni nchi itunzwayo na Bwana, Mungu wako; macho ya Bwana Mungu wako, ya juu yake, tangu mwanzo wa mwaka hata mwisho wa mwaka. |
13. | Tena itakuwa, mtakaposikiza kwa bidii maagizo yangu niwaagizayo leo, kwa kumpenda Bwana, Mungu wenu, na kumtumikia kwa mioyo yenu yote na roho zenu zote, |
14. | ndipo nitakapowapa mvua ya nchi yenu kwa wakati wake, mvua ya masika, na mvua ya vuli, upate kuvuna nafaka yako, na divai yako, na mafuta yako. |
15. | Nami nitakupa nyasi katika mavue yako kulisha wanyama wako wa mifugo, nawe utakula na kushiba. |
16. | Jitunzeni nafsi zenu, mioyo yenu isije ikadanganywa, mkageuka na kutumikia miungu mingine na kuiabudu; |
17. | hasira za Bwana zikawaka juu yenu, naye akafunga mbingu kusiwe na mvua, wala nchi isitoe matunda yake; mkaangamia kwa upesi mtoke katika nchi nzuri awapayo Bwana. |
18. | Kwa hiyo yawekeni maneno yangu mioyoni mwenu na rohoni mwenu; yafungeni yawe dalili juu ya mikono yenu, nayo yatakuwa kama utepe katikati ya macho yenu. |
19. | Nayo wafunzeni vijana vyenu kwa kuyazungumza uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo. |
20. | Tena yaandike juu ya miimo ya nyumba yako, na juu ya malango yako; |
21. | ili siku zenu zifanywe nyingi, na za vijana vyenu nao, juu ya nchi Bwana aliyowaapia baba zenu kuwa atawapa, kama zilivyo siku za mbingu juu ya nchi. |
22. | Kwa kuwa kwamba mtayashika kwa bidii maagizo haya yote niwaagizayo, kuyafanya; kumpenda Bwana, Mungu wenu, na kutembea katika njia zake zote, na kushikamana naye; |
23. | ndipo Bwana atakapowafukuza mataifa haya yote mbele yenu, nanyi mtamiliki mataifa makubwa yenye nguvu kuwapita ninyi. |
24. | Kila mahali mtakapokanyaga kwa nyayo za miguu yenu patakuwa penu; tokea hilo jangwa, na Lebanoni, na tokea mto wa Frati, mpaka bahari ya magharibi, itakuwa ndiyo mipaka yenu. |
25. | Hapatakuwa na mtu atakayeweza kusimama mbele yenu; Bwana, Mungu wenu, ataweka utisho wenu na kuhofiwa kwenu juu ya nchi yote mtakayoikanyaga, kama alivyowaambia. |
26. | Angalieni, nawawekea mbele yenu hivi leo baraka na laana; |
27. | baraka ni hapo mtakapoyasikiza maagizo ya Bwana, Mungu wenu, niwaagizayo leo; |
28. | na laana ni hapo msiposikiza maagizo ya Bwana, Mungu wenu, mkikengeuka katika njia niwaagizayo leo, kwa kuandama miungu mingine msiyoijua. |
29. | Tena itakuwa, atakapokuleta Bwana, Mungu wako, na kukutia katika nchi uendeayo kuimiliki, ndipo uiweke baraka juu ya mlima wa Gerizimu, na laana uiweke juu ya mlima wa Ebali. |
30. | Je! Haiwi ng'ambo ya Yordani? Nyuma ya njia ya machweo ya jua, katika nchi ya Wakanaani waketio katika Araba kuelekea Gilgali, kando ya hiyo mialoni ya More? |
31. | Kwani ninyi mtavuka Yordani mwingie kuimiliki nchi awapayo Bwana, Mungu wenu, nanyi muimiliki na kuketi humo. |
32. | Nanyi angalieni mzifanye amri na hukumu zote niwawekeazo leo mbele yenu. |
← Deuteronomy (11/34) → |