Deuteronomy (11/34)  

1. Kwa ajili hii mpende Bwana, Mungu wako, na kushika sikuzote mausia yake, na amri zake, na hukumu zake, na maagizo yake.
2. Nanyi leo jueni; kwa kuwa sisemi sasa na vijana vyenu, ambao hawakujua, wala hawakuona adhabu ya Bwana, Mungu wenu, ukuu wake, na mkono wake wa nguvu, na mkono wake ulionyoka,
3. na ishara zake, na kazi zake alizomfanya Farao mfalme wa Misri, na nchi yake yote, katikati ya Misri;
4. na alivyolifanya jeshi la Misri, farasi zao, na magari yao; na alivyowafunikiza maji ya Bahari ya Shamu walipokuwa wakiwaandamia, na alivyowaangamiza Bwana hata hivi leo;
5. na mambo aliyowafanyia ninyi barani, hata mkaja mahali hapa;
6. na alivyowafanya Dathani, na Abiramu, wana wa Eliabu mwana wa Reubeni; nchi ilivyofunua kinywa chake, ikawameza, na walio nyumbani mwao, na mahema yao, na kila kitu kilichokuwa hai kikiwafuata, katikati ya Israeli yote;
7. lakini macho yenu yameiona kazi kubwa ya Bwana aliyoifanya, yote.
8. Kwa hiyo yaangalieni maagizo yote niwaagizayo leo, mpate kuwa na nguvu, na kuingia mkaimiliki nchi mwivukiayo kuimiliki;
9. nanyi mpate kuzifanya siku zenu kuwa nyingi juu ya nchi Bwana aliyowaapia baba zenu, ya kuwa atawapa wao na kizazi chao, nchi imiminikayo maziwa na asali
10. Kwa kuwa nchi mwingiayo kuimiliki, si mfano wa nchi ya Misri mlikotoka, uliyokuwa ukipanda mbegu zako humo na kuinywesheleza kwa mguu wako, kama shamba la mboga;
11. lakini nchi mwivukiayo kuimiliki ni nchi ya vilima na mabonde, nayo hunyweshwa maji ya mvua ya mbinguni;
12. nayo ni nchi itunzwayo na Bwana, Mungu wako; macho ya Bwana Mungu wako, ya juu yake, tangu mwanzo wa mwaka hata mwisho wa mwaka.
13. Tena itakuwa, mtakaposikiza kwa bidii maagizo yangu niwaagizayo leo, kwa kumpenda Bwana, Mungu wenu, na kumtumikia kwa mioyo yenu yote na roho zenu zote,
14. ndipo nitakapowapa mvua ya nchi yenu kwa wakati wake, mvua ya masika, na mvua ya vuli, upate kuvuna nafaka yako, na divai yako, na mafuta yako.
15. Nami nitakupa nyasi katika mavue yako kulisha wanyama wako wa mifugo, nawe utakula na kushiba.
16. Jitunzeni nafsi zenu, mioyo yenu isije ikadanganywa, mkageuka na kutumikia miungu mingine na kuiabudu;
17. hasira za Bwana zikawaka juu yenu, naye akafunga mbingu kusiwe na mvua, wala nchi isitoe matunda yake; mkaangamia kwa upesi mtoke katika nchi nzuri awapayo Bwana.
18. Kwa hiyo yawekeni maneno yangu mioyoni mwenu na rohoni mwenu; yafungeni yawe dalili juu ya mikono yenu, nayo yatakuwa kama utepe katikati ya macho yenu.
19. Nayo wafunzeni vijana vyenu kwa kuyazungumza uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.
20. Tena yaandike juu ya miimo ya nyumba yako, na juu ya malango yako;
21. ili siku zenu zifanywe nyingi, na za vijana vyenu nao, juu ya nchi Bwana aliyowaapia baba zenu kuwa atawapa, kama zilivyo siku za mbingu juu ya nchi.
22. Kwa kuwa kwamba mtayashika kwa bidii maagizo haya yote niwaagizayo, kuyafanya; kumpenda Bwana, Mungu wenu, na kutembea katika njia zake zote, na kushikamana naye;
23. ndipo Bwana atakapowafukuza mataifa haya yote mbele yenu, nanyi mtamiliki mataifa makubwa yenye nguvu kuwapita ninyi.
24. Kila mahali mtakapokanyaga kwa nyayo za miguu yenu patakuwa penu; tokea hilo jangwa, na Lebanoni, na tokea mto wa Frati, mpaka bahari ya magharibi, itakuwa ndiyo mipaka yenu.
25. Hapatakuwa na mtu atakayeweza kusimama mbele yenu; Bwana, Mungu wenu, ataweka utisho wenu na kuhofiwa kwenu juu ya nchi yote mtakayoikanyaga, kama alivyowaambia.
26. Angalieni, nawawekea mbele yenu hivi leo baraka na laana;
27. baraka ni hapo mtakapoyasikiza maagizo ya Bwana, Mungu wenu, niwaagizayo leo;
28. na laana ni hapo msiposikiza maagizo ya Bwana, Mungu wenu, mkikengeuka katika njia niwaagizayo leo, kwa kuandama miungu mingine msiyoijua.
29. Tena itakuwa, atakapokuleta Bwana, Mungu wako, na kukutia katika nchi uendeayo kuimiliki, ndipo uiweke baraka juu ya mlima wa Gerizimu, na laana uiweke juu ya mlima wa Ebali.
30. Je! Haiwi ng'ambo ya Yordani? Nyuma ya njia ya machweo ya jua, katika nchi ya Wakanaani waketio katika Araba kuelekea Gilgali, kando ya hiyo mialoni ya More?
31. Kwani ninyi mtavuka Yordani mwingie kuimiliki nchi awapayo Bwana, Mungu wenu, nanyi muimiliki na kuketi humo.
32. Nanyi angalieni mzifanye amri na hukumu zote niwawekeazo leo mbele yenu.

  Deuteronomy (11/34)